SHIRIKA la Madini la Taifa (STAMICO) limesema mkaa mbadala wa kupikia unaojulikana kama ‘Rafiki Coal Briquettes’ unaotokana na makaa ya mawe una uwezo wa kutumiwa mara tatu zaidi ya mkaa unaotokana na kuni. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Pia limesema mradi wa uzalishaji wa mkaa huo, unatarajiwa kuwanufaisha watanzania kwa kutoa ajira na utapunguza janga la ukataji miti kwa ajili ya mkaa hivyo kuchangia kutunza mazingira.
Hayo yameelezwa leo tarehe 28 Septemba, 2022 na Meneja Masoko na Uhusiano wa Shirika hilo, Geofrey Meena wakati akitoa maelezo kwa Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini, Msafiri Mbibo.
Mbibo alitembelea banda la STAMICO katika maonesho ya kitaifa ya teknolojia ya madini yanayoendelea katika viwanja vya Bombambili mkoani Geita.
Pamoja na mambo mengine Meena amesema mkaa huo ambao unauzwa sh 1,000 kwa kilo moja, mkaa huo una faida lukuki.
“Baadhi ni pamoja na rafiki wa mazingira, kuokoa pesa nyingi zinazotumika kwenye nishati nyingine, mkaa wa mawe wakupikia unadumu jikoni kwa muda mrefu kuliko mkaa wa miti hivyo kuzidi kupunguza gharama za matumizi ya nishati hiyo, huboresha usafi wa jikoni na maeneo ya nyumbani yanayochafuliwa na mkaa wa miti,,” amesema.
Ameongeza kuwa, kutokana na manufaa ya mkaa huo, tayari STAMICO inaendelea kuweka mikakati ya kuhakikisha kuwa jamii kubwa inanufaika na inatumia mkaa huo ambao ni wazi utasaidia kufanikisha kampeni ya utunzaji wa misitu ambapo kwa kuzingatia umuhimu wake itaendelea kuleta mitambo ya kuzalisha mkaa mwingi ili kupunguza bei zaidi ya mkaa huo.
Leave a comment