SHIRIKISHO la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), limewaomba radhi wadau wa michezo, kwa tukio lililotolea jana Jumamosi, tarehe 8 Mei 2021, la kuahirishwa mchezo wa ligi kuu, kati ya watani wa jadi, Simba dhidi ya Yanga. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Mchezo huo, uliahirishwa baada ya Yanga kupinga mabadiliko ya muda wa mchezo huo, kutoka saa 11:00 jioni wa awali hadi saa 1:00 usiku.
TFF ilitangaza mabadiliko hayo takribani saa 3 kufika saa 11:00 mchezo kuanza ikiwa ni kinyume na kanuni ya 10(15) ya ligi hiyo inayotaka mabadiliko hayo, yafanyike saa 24 kabla ya mchezo.
TFF iliahirisha mchezo huo uliokuwa uchezwe Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam hadi hapo baadaye.
Leo Jumapili, Cliford Ndimbo, Ofisa Habari na Mawasiliano wa TFF, ametoa taarifa akisema, suala hilo linaendelea kushughulikiwa.
“TFF inapenda kuomba radhi kwa wadau wote, waliolipa viingilio kuingia uwanjani, waliokuwa wakisubiri kuangalia kwenye televisheni, kusikiliza redioni na watoa huduma mbalimbali,” amesema Ndimbo
Amesema, TFF imetoa maelekezo kwa Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB), kutoa taarifa ya kina kuhusu kuahirishwa kwa mchezo huo.
Pia, kushughulikia hatma ya wapenzi wa mpira wa miguu waliolipa viingilio kuingia uwanjani.
Leave a comment