SERIKALI imetangaza nafasi za ajira kwa walimu wa shule za msingi na sekondari pamoja na watumishi wa kada mbalimbali za sekta ya afya. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Nafasi hizo zimetangazwa leo Jumapili tarehe 9 Mei 2021, na Waziri Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Ummy Mwalimu, akizungumza na wanahabari jijini Dodoma.
Ummy amesema nafasi za ajira kwa walimu wa shule za msingi na sekondari ni 6,949, huku za watumishi wa kada za sekta ya afya zikiwa ni 2,726.
“Serikali imetoa kibali cha nafasi za ajira ya walimu 6,949 wa shule za msingi na sekondari na watumishi 2,726 wa kada mbalimbali za sekta ya afya,” amesema Ummy.
Waziri huyo wa TAMISEMI amesema nafasi hizo zimetangazwa kwa ajili ya kujaza pengo lililoachwa na watumishi waliokoma utumishi, kutokana na sababu mbalimbali.
“Nafasi hizo zimetangazwa ili kujaza nafasi wazi za watumishi waliokoma utumishi kutokana na sababu mbalimbali kama vifo, kuacha kazi, kufukuzwa kwenye utumishi na kustaafu,” amesema Ummy.
Ummy amesema mchakato wa kuomba ajira hizo umekamilika, na kwamba wahitaji wanaweza kuomba nafasi hizo kuanzia leo hadi tarehe 23 Mei 2021.
“Taratibu za kuanza mchakato wa kuomba ajira umekamilika, waombaji wenye nia wanaweza kutuma maombi yao kwa njia ya mtandao kupitia kiunganishi cha ajira TAMISEMI, kuanzia leo tarehe 9 hadi 23 Mei, 2021,” amesema Ummy.
Leave a comment