KESI iliyofunguliwa na wabunge viti maalum 19, kupinga kuvuliwa uanachama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), imekwama kusikilizwa baada ya shahidi kushindwa kufika mahakamani akidaiwa kuwa mgonjwa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Kesi hiyo Na. 36/2022, ilipangwa kusikilizwa leo tarehe 26 Julai 2023, katika Mahakama Kuu, Masjala Kuu, jijini Dar es Salaam, mbele ya Jaji Cyprian Mkeha.
Wabunge hao 19, wakiongozwa na Halima Mdee, wamefungua kesi dhidi ya Chadema, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), wakiomba mahakama ifanye mapitio dhidi ya mchakato uliotumika kuwafukuza ndani ya chama hicho, kama ulikuwa halali au batili.
Akizungumza baada ya kesi hiyo kuahirishwa, Wakili wa Chadema, Hekima Mwasipu, amedai shahidi ambaye ni Mjumbe wa Bodi ya Wadhamini ya chama hicho, Marry Joackim, aliyepangwa kuuulizwa maswali ya dodoso na mawakili wa kina Mdee, ameshindwa kufika mahakamani kwa madai kuwa mgonjwa.
Pia, Wakili Mwasipu alidai shahidi mwingine ambaye alipangwa kuulizwa maswali hayo, Ahmed Rashid Hamis, ameshindwa kufika mahakamani hapo leo kwa kuwa yuko safarini akitokea visiwani Zanzibar, kuja Dar es Salaam.
Kufuatia sababu hizo, Jaji Mkeha ameahirisha kesi hiyo hadi kesho tarehe 27 Julai mwaka huu.
Mdee na wenzake wamefungua kesi hiyo wakipinga uamuzi wa Chadema kuwafukuza, wakidai hawakupewa nafasi ya kusikilizwa.
Chadema waliwafukuza wabunge hao wakiwatuhumu kwa usaliti kufuatia uamuzi wao wa kukubali kuapishwa kuwa wabunge viti maalum bila ridhaa yake.
Leave a comment