SERIKALI kwa mara ya kwanza imeanzisha utaratibu wa ‘Samia Suluhu Super specialist program’ wa kusomesha madaktari bingwa zaidi ya 400 ili kukabiliana na upungufu wa wataalaam hao katika hospitali mbalimbali nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Hayo yamebainishwa jana bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu wakati akijibu swali la Mbunge wa Tabora Mjini, Emanuel Mwakasaka (CCM).
Mwakasaka alihoji ni lini serikali itapeleka madaktati bingwa 11 katika hospitali ya rufaa Kitete kwani mwaka jana alihoji suala hilo la kujibiwa kwamba wangepelekwa mwaka jana Novemba.
Awali Naibu Waziri wa Afya, Godwin Mollel alijibu ndivyo sivyo hali uliyomlazimu Waziri Ummy kufafanua jibu la swali hilo.
Ummy Mwalimu alisema madaktari hao wanasoma kwa utaratibu alioupa jina la Set kwamba kama alikuwa daktari wa usingizi anakwenda kusomea udaktari bingwa wa eneo hilohilo.
“Pongezi kwake Mheshimiwa Rais Samia, kwa kutenga bajeti Sh biioni 8 kwa ajili ya kusomesha wataalam kama wa usingizi, nesi, ndani na nje ya nchi,” alisema.
Alisema changamoto ni madaktari hao kurejea kwenye maeneo yao ya kazi baada ya kusomeshwa hivyo serikali itaendelea kuwahasisha kwenda mikoani kutoa huduma.
Kutokana na hali hiyo Spika wa Bunge, Tulia Ackson alisema kwa kuwa wanasomeshwa kwa fedha za serikali, wapewe masharti kwamba lazima warudi walipofanyia kazi.
Aidha, Ummy Mwalimu alisema wamefikia hatua ya kusomesha madaktari hao kwani awali walitangaza nafasi lakini madaktari bingwa wakakosekana sokoni.
Leave a comment