SERIKALI imeanza kutekeleza maombi ya Mbunge wa Musoma Vijijini, Prof. Sospeter Muhongo (CCM) ya kupeleka vifaa tiba na watumishi katika kituo kipya cha afya cha Rukuba, ilichojenga kwa kushirikiana na wananchi wa kisiwa hicho. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mara…(endelea).
Hivi karibuni Serikali ilipeleka vifaa tiba vyenye thamani ya zaidi ya Sh. 100 milioni, kituoni hapo, ikiwa ni zaidi ya miezi miwili tangu Prof. Muhongo awasilishe maombi hayo.
Akizungumza baada ya kupokea vifaa tiba hivyo, Prof. Muhongo ameishukuru Serikali huku akiiomba iongeze watumishi ikiwemo madaktari wa upasuaji na dawa.
“Kwa sababu tuna kituo cha afya hapa, wafanyakazi wa kutoa huduma mbalimbali za afya wapo wachache sana, idadi inabidi iongezeke tunaomba iongezeke hasa kwenye madaktari watakaofanya upasuaji na wauguzi ,”amesema Prof. Muhongo.
Aidha, Prof. Muhongo amesema utoaji huduma za afya ndani ya jimbo hilo unaendelea kuboreshwa na kuimarika na kwa sasa lina hospitali ya halmashauri yenye hadi ya hospitali ya wilaya. Vituo vya afya sita na zahanati 42.
Mnamo Julai 2023, Prof. Muhongo aliiomba Serikali ipeleke vifaa tiba na watumishi katika kituo hicho, ili kuwaondolea wananchi adha ya kusafirisha wagonjwa hususan mahututi na wajawazito wanaotaka kujifungua kwenda katika hospitali za mjini kwa kutumia mitumbwi, kitendo kinachohatarisha maisha yao.
Baadhi ya wananchi wameishukuru Serikali kwa kutoa fedha kiasi cha Sh. 500 milioni kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho na kupeleka vifaa tiba, wakisema hatua hiyo itawasaidia kupata huduma ya afya karibu.
Miongoni mwa vifaa vilivyopokelewa ni vya kusaidia kina mama wajawazito kujifungua na kuhudumia watoto wanaozaliwa na matatizo mbalimbali ikiwemo kukosa hewa ya oksijeni na kunywa maji.
Leave a comment