SERIKALI imeagiza uchunguzi ufanyike ili kubaini chanzo cha maporomoko ya udongo ya Mlima Hanang mkoani Manyara, yaliyosababisha mauji ya watu zaidi ya 50 na kujeruhi wengine 85. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Agizo hilo limetolewa leo tarehe 4 Desemba 2023 na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, kwenda kwa Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, alipowasili mjini Katesh, wilayani Hanang, kwa ajili ya kushughulikia janga hilo lililotokea usiku wa kuamkia jana Jumapili.
Amesema uchunguzi huo utakapokamilika utaonesha sababu za mlima huo kuporomosha udongo.
“Wizara ya Madini tumelazimika kuileta kwa haraka tunataka tuone ni nini hiki, aina gani ya udongo huu? mwamba kama ambavyo ilifanyika Mtwara 1990 na tukagundua kulikuwa na mwamba ulilegea hapa baada ya uchunguzi wao tutapata taarifa ni nini hasa kilisababisha hiki,” amesema Waziri Majaliwa.
Hadi sasa Serikali imetuma vikosi vya uokoaji ikiwemo wanajeshi 300 wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), kwa ajili ya kusaidia shughuli za uokoaji.
Waziri Majaliwa ameagiza vyombo vya ulinzi na usalama viimarishe ulinzi katika eneo lililoathirika ili kulinda raia na mali zao, huku akitaka watalaamu wabaki hadi pale hali itakapotengemaa.
Leave a comment