RAIS wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, amekatisha ziara yake za kikazi jijini Dubai kwa ajili ya kurejea nchini kushughulikia maafa yaliyotokana na maporomoko ya udongo ya Mlima Hanang usiku wa kuamkia jana kwenye Mji wa Katesh, mkoani Manyara. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa ya Rais Samia kukatisha ziara ya kushiriki mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Mabadaliko ya Tabianchi (COP28), imetolewa leo tarehe 4 Desemba 2023 na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais-Ikulu, Zuhura Yunus.
“Rais Samia amekuwepo Dubai kwa ajili ya mkutano wa COP28, ameamua kufupisha safari hiyo na kurejea nchini haraka iwezekanavyo ili kushughulikia kwa karibu janga hilo,” imesema taarifa ya Yunus.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Rais Samia amemuagiza Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, kuhakikisha Serikali inagharamia mazidi ya watu wote waliopoteza maisha kutokana na janga hilo.
“Pia, Rais Samia ametaka majeruhi wote ambao wapo kwenye hospitali mbalimbali wapate matibabu yote yanayostahili kwa gharama za Serikali, huku vyombo vya ulinzi na usalama vikiendelea kutoa msaada wa dharura na uokoaji,” imesema taarifa hiyo.
Katika hatua nyingine, Rais Samia ameagiza wananchi waliopoteza makazi yao kufuatia janga hilo, watafutiwe makazi ya muda.
Tayari Waziri Majaliwa ameshawasili mkoani Manyara, ambapo amesema janga hilo limeleta athari mbalimbali, ikiwemo uharibifu wa miundombinu za nyumba na barabara, nyumba, magari na mali nyingine.
Hadi sasa mamlaka za Serikali zimeripoti watu zaidi ya 50 wamepoteza maisha huku wengine zaidi ya 80 wakijeruhiwa.
Shughuli za uokoaji na uokoaji zinaendelea kufanywa na vitengo vya uokoaji pamoja na wanajeshi wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) 300 waliopelekwa mkoani humo kwa ajili ya kutoa msaada.
Leave a comment