MTANDAO wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), imeitaka Serikali kupiga marufuku malori ya mizigo kutembea barabarani wakati wa mchana ili kulinda maisha ya raia yaliyoko hatarini kutokana na ajali, huku ikisisitiza kuwa, isipochukua hatua hiyo itaifikisha mahakamani. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Msimamo huo ulitolewa jana Jumapili na Mratibu wa Kitaifa wa THRDC, Onesmo Olengurumwa, baada ya watu 25 kufariki dunia na wengine 21 kujeruhiwa katika ajali ya gari iliyohusisha lori na magari matatu, kutokea tarehe 24 Februari mwaka huu.
Olengurumwa amemtaka Waziri wa Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa, kuhakikisha utaratibu wa malori ya mizigo kutembea usiku, unatekelezwa kikamilifu.
“Malori wakati mwingine ni mabovu yanashindwa kumudu barabara kama iliyotokea katika ajali ya huko Arusha, kwa hiyo natoa pole kwa wafiwa wote lakini tunatoa wito kwa Wizara zinazohusika zihakikishe kwamba malori hayatembei usiku, vinginevyo tukiona ajali zinaendelea kutokea tutakwenda Mahakamani kuchukua hatua kuona kwamba tunatetea haki ya kuishi wananchi wa Tanzania,” alisema Olengurumwa na kuongeza:
“Tunashauri tutanue na tuboreshe barabara zetu ziwe imara na tutumie usafiri wa reli kwa biashara kubwa ili kupunguza zaidi matumizi ya barabara kwa magari makubwa. Barabara iwe zaidi matumizi ya raia na shughuli za kila siku hii itasaidia kuondoa changamoto zinazojitokeza barabarani.”
Miongoni mwa watu waliopoteza maisha katika ajali hiyo ni wanawake 10, wanaume 14 na mtoto mmoja wa kike. Wapo raia wa kigeni kutoka Kenya, Togo, Madagascar, Burkina Faso, Marekani na Afrika Kusini.
Leave a comment