MSHITAKIWA namba moja katika kesi namba mbili yam waka 2022 ya uhujumu uchumi na matumizi mabaya ya ofisi, Lengai Ole Sabaya, ametinga mahakama ya hakimu mkazi moshi akiwa na bandeji kichwani. Anaripoti Mwandishi Wetu, Moshi…(endelea)
Sabaya ambaye amewahi kuwa mkuu wa wilaya ya Hai amefika mahakamani hapo leo Ijumaa tarehe 29 Julai, 2022 ambapo mawakili wake wameileza mahakama kuwa mteja wao ana hali mbaya baada ya kufanyiwa upasuaji Julai 27 mwaka huu.
Akiwasilisha hoja hiyo wakili wa Sabaya, Fridolin Bwemelo, ameieleza mahakama kuwa mteja wao anahitaji uangalizi maalumu kutokana na kuwa upasuaji alifanyiwa ni mkubwa.
Mawakili wa Sabaya waliieleza mahakama iharakishe usikilizwaji wakesi hiyo kwani upande wa mashitaka walishaeleza kuwa upelelezi umekamilika.
Hata hivyo wakili upande wa mashtaka Sabitina Mcharo aliieleza mahakama hiyo kuwa upelelezi bado haujakamilika na kwamba wanasubiri kibali kutoka kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali cha kuipa uwezo mahakama hiyo kuendelea kuisikiliza kesi hiyo.
Hakimu mkazi wa mahakama hiyo, Elibariki Philly aliahirisha kesi hiyo mpaka Agosti 12 mwaka huu.
Sabaya na wenzake wanne wanakabiliwa na mashtaka saba likiwamo la uhujumu uchumi na matumizi mabaya ya ofisi wakati akiwa Mkuu wa wilaya hiyo.
Washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni Sylvester Nyegu, John Aweyo, Nathan Msuya na Antero Assey.
Leave a comment