AJALI mbaya ya gari imetokea leo Jumatano katika barabara kuu ya Tunduma – Mbeya (TANZAM) maeneo ya Mpakani – Chapwa wilayani Momba mkoani Songwe na kusababisha vifo vya watu sita na wengine kadhaa kujeruhiwa. Anaripoti Ibrahim Yassin,Songwe …(endelea)
Akithibitisha kutokea kwa ajali hiyo iliyotokea leo tarehe 5 Julai 2023, Kamanda wa polisi mkoani Songwe, Teopista Mallya amesema ajali hiyo imetokea muda wa saa 12 .30 asubuhi.
Amesema chanzo cha ajali hiyo ni gari namba T.867 DAQ/ T.612 CXH aina ya Faw iliyokuwa ikiendeshwa na dereva ambaye amekimbia, ililigonga gari lenye namba za usajili T. 712 DXH aina ya Mitsubishi Fuso iliyokuwa ikiendeshwa na Wille Mgala.
Amesema baada ya gari hiyo aina ya Faw kuigonga Fuso, pia iliigongana Bajaji yenye namba za usajili MC 123 DUS na hatimaye gari yenye namba za usajili T.851 CZX Toyota Haice iliyokuwa ikiendeshwa na Elifaret Jackson Majera.
Amesema ajali hiyo imesababisha vifo vya watu sita papo hapo na majeruhi kadhaa ambao wamepelekwa katika Hospitali ya Tunduma.
Amewataja watu hao kuwa ni Isack Kasebele (28) mkazi wa Mwaka, Baraka Lutufyo (23) Mkazi wa Chapwa, Fred Karagwe (28) mkazi wa Mpemba, Emmanuel Mlai (24) mkazi wa Tunduma, John Kapizo (35) mkazi wa Majengo, na mwingine jina lake halikutambulika.
Aidha, amewataja majeruhi kuwa ni Hassan Mwambazo (45) mkazi wa Darren es Salaam, Zainabu Hassan (43) mkazi wa Mpakani na wa tatu ni Oliver Ngusa (38) mkazi wa Chapwa.
Amesema chanzo cha ajali ni gari hiyo aina ya Faw kufeli breki na kugonga magari mengine ikiwemo Bajaji.
Amesema jitihada za kumtafuta dereva wa gari iliyosababisha ajali anatafutwa kwani ametoroka baada ya ajali hiyo.
Leave a comment