RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amesema panapotokea uvunjifu wa amani mara nyingi ni pale haki inapopotezwa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Jumatano tarehe 1 Februari wakati akihitimisha kilele cha maadhimisho ya wiki ya Sheria jijini Dodoma.
Rais Samia amesema kuwepo amani nchini ni chachu kubwa ya maendeleo ya kuichumi lakini hata kijamii na kisiasa pia.
“Nchi yetu imejengwa kwa misingi inayozingatia haki, inayodumisha amani na ambayo inaweza kupotea endapo migogoro inayofikishwa mahakamani haitatuliwi kwa haraka,” amesema Rais Samia na kuongeza;
“Ukiangalia panapotoeka uvunjifu wa amani mara nyingi panakuwa haki imepotezwa na haki ikipotezwa basi amani inakuwa haipo kwahiyo tujitahidi sana haki ipatikane mapema ili amani ya nchi yetu iendelee kutunzwa na kuendelezwa.”
Mkuu huyo wa nchi ametoa wito kwa vyombo vya sheria hususani mahakama kuhakikisha inatoa haki kwa haraka na kutaka sheria zote zinazosababisha mchakato wa utoaji haki kuwa mrefu zirekebishwe.
“Nitoe wito kwa mahakimu, majaji na wadau katika sekta ya sheria kupitia upya taratibu ambazo mashauri hupitia ili kuzifupisha kwa lengo la kuhakikisha upatikanaji wa haki unafanyika kwa haraka,” amesema.
Amesema kama Serikalini wanafanya jitihada kubwa kuendelea kukuza upatikanaji wa haki kwa wananchi kwa kuipitia upya mifumo iliyopo.
“Kama mlivyoona jana nilizindua tume ya kuangalia mienendo ya taasisi za haki jinai inayoongozwa na mwenyekiti Jaji Othmana Chande na makamu wake Ombeni Sefue hii itafanya kazi kwa mienzi minne kuangalia mifumo ya haki na utatuzi wa migogoro inaimarishwa si tu kwaajili ya linda amani bali pia kukuza uchumi,” amesema.
Leave a comment