RAIS Samia Suluhu Hassan, amesema hapo awali alikuwa anaogopa kuingia katika majengo ya mahakama na polisi, akieleza kuwa alihisi huenda akageuziwa kibao endapo atafikisha malalamiko yake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Mkuu huyo wa nchi ametoa kauli hiyo leo tarehe 31 Januari 2023, Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma, akizindua tume aliyoiunda kuangalia jinsi ya kuboresha utendaji wa taasisi za haki jinai nchini.
“Mimi kama mimi lile jengo la mahakama naliogopa, ya polisi naogopa sababu nikiingia polisi hata kama nina jambo kwenda kulishtaki mimi, nilikuwa naogopa huko nyuma kwamba niende polisi nikashtaki kwa mba nimefikwa na hili watanigeuzia hivyo siendi. Au uniambie sijui fulani ana kesi nenda mahakamani hataka kama kesi siyo yangu siendi,” amesema Rais Samia.
Rais Samia ameitaka tume hiyo kuangalia mahusiano kati ya taasisi za haki jinai na wananchi, kama yako vizuri au lah.
“Mkaangalie taasisi hizo na raia, raia wanazionaje? Kwa hiyo wangapi wanaogopa majengo hayo badala ya kuona kwamba ni maeneo ya kusaidiwa kupata haki zao? Watu tunaogopa kua-proach hayo majengo kwa hiyo twendeni tukatizameni kuna nini,” amesema Rais Samia.
Katika hatua nyingine, Rais Samia ameiagiza tume hiyo ikaangalie namna ya uwepo wa mifumo ya kidigitali itakayosaidia utendaji kazi kati ya Jeshi la Polisi na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), ili kuepusha vitendo vya watuhumiwa kubambikiwa makosa.
“Vyombo vyetu vya kusimamia haki inatakiwa akikamatwa mtu Polisi akitoa statement yake isomeke mpaka kwa DPP aweze kui-access na aisome Polisi asipate muda wa kubadilisha lakini the way mtu anavyoambiwa toa statement yako ndivyo vyenyewe au polisi anaweka ya kwake kisha anamuwekea kirungu saini hapa,” amesema Rais Samia.
Katika hatua nyingine, Rais Samia ameigiza tume hiyo kupitia utendani wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), akisema kwamba kuna baadhi ya maafisa wake wamekuwa wakiwabambikia watu wasiokuwa na hatia kesi.
“Tumekuwa na kesi kadhaa vijana wetu hawa wanakwenda kumtegeshea mtu paa, halafu wanakwendaa wanazunguka wanaona kikundi cha watu hiko hapo, tunakuja kukupekua ana madawa ya kulevya, mkuu tumemkamata kumbe wamezitegesha wenyewe wanachepusha haki za watu, wanatia hatiani watu wasiopaswa kutiwa hatiani, twendeni tukawatizame,” amesema Rais Samia.
Leave a comment