RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema mabadiliko madogo ya Baraza la Mawaziri aliyoyafanya hivi karibuni, si adhabu bali yanalenga kuimarisha maendeleo ya nchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar…(endelea).
Mkuu huyo wa nchi, ametoa kauli hiyo leo tarehe 1 Septemba 2023, akiwaapisha viongozi aliowateua hivi karibuni, ikiwemo mawaziri na manaibu waziri, Ikulu ndogo visiwani Zanzibar.
“Lakini la pili mjue tu kwamba, mabadiliko haya ni adjustment. Maendeleo lazima yawe na bandika bandua, kaza nati fungua nati toa nati hii weka hapa. Ndiyo maana ya mabadiliko haya. Lakini tukikaa wenyewe nitawaeleza kwa undane. Nataka nisisitize kwamba, mabadiliko haya si adhabu, ni mabadiliko ya kawaida kuimarisha maeneo yetu,” amesema Rais Samia.
Rais Samia amewataka viongozi kutii viapo vyao, pamoja na kujenga mahusiano mazuri na watendaji wengine katika wizara walizoteuliwa kufanyia kazi.
“Nataka nisisitize kwamba, mabadiliko haya si adhabu. Ni mabadiliko ya kawaida ya kuimarisha maeneo yetu. Ninachotarajia kwenu ni commitment kwenye kazi zenu. Ninyi ni watumishi wa umma sasa kuna mwingine akipata uteuzi sasa atanijua mimi nani? Kwa hiyo sisi ni watumishi wa watu na katika utumishi wa watu mahusiano ni jambo zuri sana,” amesema Rais Samia.
Rais Samia amesema “Naombeni sana upole si ujinga hata kidogo, upole saa nyingine ndiyo maarifa. Unatulia, unafikiri jambo mara mbili tatu kabla hujatoa maamuzi. Kwa hiyo naomba mkatulie mtumikie watu.”
Aidha, Rais amesema baada ya mawaziri aliowateua kuapishwa, atafanya nao kikao kazi kwa ajili ya kuwapa maelekezo ya namna ya kufanya kazi.
“Mawaziri na manaibu hamtaondoka, tutakutana hapa ili tuweze kuchambuana vizuri tuelezane, mkiondoka hapa mjue mnakwenda kufanyaje,” amesema
Katika hatua nyingine, amewataka mawaziri wapya kuhakikisha wanaleta mabadiliko katika wizara walizopangiwa.
“Kwa wapya, Jerry, Kapinga, Kihenzile, Kitandula, ninyi ni wapya kabisa. Nadhani mnayaona yanayotokea bungeni na mmekuwa mkipaza sauti kubwa kwa mawaziri bungeni. Yale mliyokuwa mkiyapazia sauti mnakwenda kuyafanyia nyinyi. Tunatarajia mcheze kweli kweli mlete yale mabadiliko mliyokuwa mkiyahoji kule,” amesema Rais Samia.
Leave a comment