RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, ameonesha kutoridhishwa na baadhi ya wakuu wa mikoa na wilaya ambao wanashindwa kutatua changamoto za wananchi zilizokuwa ndani ya uwezo wao, kitendo alichosema kinaweza wapa wapinzani nafasi ya kuchaguliwa kwa kuwa wananchi wataona Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimezipuuza shida zao. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Akizungumza katika hafla ya kuwaapisha viongozi aliowateua hivi karibuni, leo tarehe 13 Machi 2024, Ikulu jijini Dar es Salaam, Rais Samia amesema inabidi wasaidizi wake hao watatue changamoto za wananchi badala ya kumsubiria Katibu Mwenezi wa CCM, Paul Makonda, apite.
“Nataka niwakumbushe ninyi ndio marais wa maeneo yale, shida yoyote ya eneo lile ni shida yako kama nilivyo mimi nina mawaziri na makatibu wakuu na ninyi kule mna wa kuwasaidieni kazi sasa tukiwa tunakwenda tu mambo yanatokea mpaka apite Makonda watu walie hivyo sivyo naombeni kila mmoja akasimame kwenye eneo lake,” amesema Rais Samia.
Rais Samia amewataka wakuu wa mikoa na wilaya kutatua kero zinazowakabili wananchi, huku akiwahimiza kuwa tayari kufanya kazi usiku na mchana kuhakikisha wananchi wao wanakuwa salama.
“Jengine ni kusimamia kero za wananchi, Makonda amezunguka mmeona mfano wa wananchi wana kero kadhaa nyingine ni nyepesi za kutatuliwa kule chini lakini hawasikilizwi na wasiposikilizwa zile ndizo kura zetu. Wasiposikilizwa au msipowasikiliza akipita mwingine akimwambia mimi nikiingia nitawasikiliza watatamka kwamba sisi tuliopo hatuwasikilizi huko ndiko kwenye ushindi,” amesema Rais Samia.
Leave a comment