RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amekutana na kuzungumza na Mjumbe Maalum wa Boris Jonson, Waziri Mkuu wa Uingereza katika masuala ya biashara kati ya Uingereza na Tanzania, Lord John Walney. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Ni jana Jumapili, tarehe 31 Oktoba 2021, katika mji wa Glasgow, Scotland
ambapo Walney alikutana na Rais Samia kujitambulisha akiwa na jukumu la kuwa kiungo kati ya nchi hizo mbili kuhusu masuala ya biashara, uwekezaji na utalii.
Amesema, kukutana kwake na Rais Samia kumempa fursa ya kujua vipaumbele vya Serikali ya Tanzania ambavyo vitamwezesha kuwashawishio wafanyabiashara wa Uingereza kuwekeza katika sekta ya biashara na utalii nchini Tanzania.
Kwa upande wake, Rais Samia amemshukuru Walney kwa uamuzi wake wa kukutana naye na kujitambulisha kwake na kumueleza Serikali ya Tanzania ipo tayari kushirikiana na Serikali ya Uingereza katika kuchochea biashara baina ya nchi mbili hizo.
Rais Samia amesema, Serikali ya Uingereza na Tanzania zimekuwa na ushirikiano wa kibiashara kwa muda mrefu ambapo Uingereza ni moja kati ya nchi zinazoongoza kuwekeza nchini Tanzania, hivyo kupitia mjumbe huyo kutaongeza fursa zaidi za kibiashara katika kukuza ushirikiano wa uchumi na Uingereza.
Taarifa ya mazungumzo hayo, imetolewa na Jaffar Haniu, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu.
Rais Samia yupo nchini Scotland, kuhudhulia mkutano wa 26 wa Umoja wa Mataifa unaojadili athari za mabadiliko ya tabianchi (COP26) ambapo kesho Jumanne, tarehe 2 Novemba 2021, atakuwa miongoni mwa viongozi watakaohutubia mkutano huo.
Leave a comment