MSEMAJI Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa amesema Serikali haijarudi Dar es Salaam bali imehamia moja kwa moja Dodoma. Anaripoti Mwandishi Wetu, Iringa … (endelea).
Amesema katika kuthibitisha hilo, tayari watumishi 18,000 wa umma wameshahamia Dodoma, hii ikiwa ni pamoja na Rais Samia Suluhu, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, mawaziri, manaibu mawaziri na yeye mwenyewe.
Msigwa ametoa kauli hiyo leo taerehe 31 Oktoba, 2021 Mjini Iringa mkoani Iringa wakati akizungumza na waandishi wa habari pamoja na umma wa Watanzania kama ilivyo utaratibu wake wa kuzungumza na watanzania kila wiki.
Akijibu swali la mmoja wa waandishi wa habari waliohudhuria mkutano huo, Msigwa amesema, “Kuhusu kuhamia Dodoma serikali yote imehamia Dodoma, usimsingizie mjomba wangu Spika Job Ndugai kuwa Serikali imehamia Dar es Salaam… hapana!
“Alichosema Spika ni kwamba baadhi ya shughuli zimerudishwa Dar es Salaam, sio kwamba Serikali imerudi Dar es Salaam.
“Serikali yote ipo Dodoma, Rais, Waziri Mkuu, Mawaziri, Manaibu Mawaziri na Msigwa wote makazi yao yapo Dodoma. Nikitoka hapa Iringa narudi Dodoma,” amesema.
Amesema awali Serikali ilijenga majengo ya muda kwenye wizara zote baada ya kila moja kupatiwa Sh bilioni moja.
“Hivi ninavyozungumza tunakwenda kujenga majengo 24 yenye ghorofa sita hadi 11. Serikali imetoa Sh bilioni 600 kwa ajili ya kuhakikisha wizara zote zinakuwa na majengo ya kudumu ya wizara.
“Tuko Dodoma… Mchezo huo umekwisha, isipokuwa kwa sasa baadhi ya shughuli zilikuwa zinafanyika Dar es Salaam kutokana na uhitaji ila wito uliotolewa na Spika umepokewa na Serikali unafanyiwa kazi na bila shaka mambo yatakwenda vizuri,” amesema.
Leave a comment