RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ameshauriwa kuongeza juhudi katika dhamira yake ya kuimarisha usawa wa kijinsia na kumuinua mwanamke kiuchumi, ili kuondoa dhana potofu kwamba kundi hilo halina uwezo wa kuleta maendeleo kwa Taifa. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Wakizungumza katika nyakati tofauti na MwanaHALISI Online, wadau wanaotetea haki za binadamu na masuala ya jinsia, wamesema tangu alipoingia madarakani Machi 2021, kufuatia kifo cha mtangulizi wake, Hayati John Magufuli, Rais Samia amekuwa akitekeleza masuala mbalimbali kwa lengo la kuwainua wanawake katika uongozi.
Hata hivyo, wadau hao wameeleza kuwa, jitihada hizo zinapaswa kwenda sambamba na kutekeleza mikakati inayolenga kumuinua mwanamke kijamii na kiuchumi.
Mdau wa masuala ya haki za binadamu Zanzibar, Shadida Omar, amemuomba Rais Samia aendelee kuongeza juhudi katika kuwainua wanawake, ikiwemo kwa kuhakikisha vikundi vya maendeleo ya kina mama vinaongezeka na sheria kandamizi dhidi ya mwanamke zinaondolewa.
Aidha, Shadida amesema Rais Samia amekuwa na mchango mkubwa katika kuwaletea wanawake maendeleo kupitia njia mbalimbali, ikiwemo katika teuzi za nafasi za uongozi Serikalini, pamoja na kuwahimiza kuwa na desturi ya kuinuana badala ya kuwekeana vikwazo.
“Kawaweka katika sehemu tofauti za ajira, kama haitoshi ajira ambazo wengi wetu tulikuwa na imani ya kwamba mwanamke hawezi kuongoza mfano aliwahi mteua Dk. Stergnomena Tax, kuwa Waziri wa Ulinzi. Lakini huu ni mwaka wa pili hakuna kurudi nyuma, kachagua wanawake kuwa mawaziri na manaibu waziri mbalimbali, nakatibu wakuu wakurugenzi na maafisa mbali mbali,” amesema Shadida.
Naye Kaimu Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake la Chama cha Demokrasia na Maendeleo (BAWACHA), Sharifa Suleiman, amesema ili Rais Samia awainue zaidi wanawake, anatakiwa anatakiwa apanue wigo katika masuala yanayojenga ili waweze kuwa viongozi wazuri wa kisiasa na kijamii.
“Mchango wa Rais Samia katika kuwainua wanawake sio mbaya, lakini kama ana nia ya dhati kuwanyanyua wanawake kuweza kufanya masuala ya uongozi inabidi uwafungulie majukwaa ya kisiasa. Awaachie vyama vya siasa vya upinzani kufanya mikutano ya hadhara, hapo ataweza kuwajenga kisiasa kumiliki jukwaa na kugombea nafasi za uongozi,” amesema Sharifa na kuongeza:
“Wasipofanya mikutano ya hadhara hizo fursa za kujijenga kiuongozi hawatazipata. Bado tunamuomba aliangalie suala hilo kwa macho mawili kama alivyoahidi kwamba ikifika Desemba 2022, atafungulia mikutano ya hadhara.”
Kwa upande wake Mratibu wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), Onesmo Olengurumwa, amesema bado jitihada zaidi zinahitajika kuwakomboa wanawake dhidi ya changamoto wanazokabiliana nazo.
“Kuna mambo mengi Rais Samia ameyafanya mazuri katika haki za binadamu hasa upande wa jinsia, katika teuzi mbalimbali tukizona zikizingatia jinsia na makundi mengine. Bado tunahitaji kuona jitihada zaidi. Usawa tunaozungumzia uangalie maeneo mengine ya kijamii na sio tu kiuongozi, maana yake tuboreshe nafasi ya mwanamke katika maeneo ya kijamii, kiuchumi na kisiasa,” amesema Olengurumwa.
Leave a comment