RAIS Samia Suluhu Hassan, ameondoa zuio la mikutano ya hadhara ya vyama vya siasa, lililowekwa na mtangulizi wake, Hayati John Magufuli, kwa maelezo kwamba kuipa nafasi Serikali kufanya kazi ya kuijenga nchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Rais Samia ameondoa marufuku hiyo leo Jumanne, tarehe 3 Januari 2023, akizungumza na viongozi wakuu wa vyama vya siasa vya upinzani Tanzania, Ikulu jijini Dar es Salaam.
Rais Samia amesema Serikali itawakuwa na wajibu wa kulinda mikutano hiyo ili ifanyike kwa amani, huku akivitaka vyama vya siasa kutoa taarifa juu ya ratiba ya mikutano hiyo.
“Nianze na la mikutano ya hadhara, hii ni haki kwa sheria zetu. Ni haki ya vyama kufanya mikutano yao ya hadhara na kwa bahati taarifa zote mbili zimeibuka kama ni jambo muhimu sana. Uwepo wangu leo mbele yenu ni kuja kutoa ruhusa, kuja kutangaza kwamba lile tangazo la kuzuia mikutano ya hadhara sasa linaondolewa,” amesema Rais Samia.
Aidha, Rais Samia amevitaka vyama hivyo kufanya mikutano ya hadhara kwa kuzingatia sheria za nchi, pamoja na kufanya siasa za kistaarabu na zenye kuibua hoja zitakazoleta maendeleo ya Taifa.
“Wajibu wenu vyama ni kufuata sheria zinavyosema, ni kufuata kanuni zinavyosema ndiyo wajibu wenu. Lakini kama waungwana wastaarabu niwaombe sana, tunatoa ruhusa ya vyama vya siasa twendeni tukafanye siasa za kistaarabu, za kupevuka. Tukafanye siasa za kujenga na si kubomo, kurudi nyuma,” amesema Rais Samia.
Katika hatua nyingine, Rais Samia amesema Serikali yake na Chama chake cha Mapinduzi (CCM), ni muumini wa kukubali kukosolewa kwa kuwa inapata nafasi ya kujua changamoto zilizopo kwa ajili ya kufanyiwa kazi.
Leave a comment