RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema kama historia ya Hayati Edward Lowassa ndani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ingewekwa katika wasifu wake, mwenyekiti wa chama hicho Taifa, Freeman Mbowe asingepata cha kuongea katika mazishi yake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Jumamosi, katika mazishi ya Hayari Lowassa, yaliyofanyika nyumbani kwake Monduli, mkoani Arusha, baada ya Mbowe kusema amesikitishwa na kitendo cha wasifu huo kutojumuisha safari ya mwanasiasa huyo ndani ya Chadema.
Mkuu huyo wa nchi alitoa kauli hiyo wakati akielezea sifa za Lowassa katika tasnia ya siasa, ambapo alisema enzi za uhai wake alifanikiwa kuwalea vijana wengi kisiasa kitendo kilichomuongezea umaarufu na ushawishi hadi kupelekea kupata kura nyingi alipogombea urais wa Tanzania kupitia Chadema mwaka 2015.
“Lowassa alikuwa kiongozi, alilea na kukuza wanasiasa vijana wengi ambao wanaendelea kulitumikia taifa. Sifa hii ya ulezi na kuongoza vijana katika maisha yao ya kisiasa ilimjengea umaarufu na matokeo makubwa ndiyo maana alichosema mdogo wangu Freeman yale matokeo ya kura ni kwa sababu hii alijenga umaarufu mkubwa sana yeye mwenyewe binafsi,” amesema Rais Samia.
Rais Samia amesema “Pia tungeyasema sisi usingepata la kusema ndugu yangu ndiyo maana umekuja umepata la kusema, kwa hiyo nakushuru sana.”
Baada ya kumjibu Mbowe, katika hotuba yake Rais Samia alieleza mapito ya kisiasa ya Lowassa, huku akielezea namna alivyojiunga na Chadema.
“Nimezungumzia pia suala la ustahimilivu ambalo ni jambo lingine la kujifunza kwa maisha ya Lowassa, katika mapito yake ya kisiasa aliwahi kuhama kutoka CCM kwenda Chadema, hapo Mbowe vipi? ambako aliteuliwa kuwa mgombea urais kwenye uchaguzi wa 2015,” amesema Rais Samia.
Amewataka wanasiasa kuiga mfano wa Lowassa wa kunadi sera zao bila kutukana, kukejeli na kudhalilisha wengine.
“Kama mlivyosikia Lowassa alichipukia na kulelewa Chama Cha Mapinduzi , hata hivyo alivyofanya maamuzi ya kuhamia chama kingine aliendelea kunadi sera zake na kuifafanua dhana yake ya safari yake ya matumaini bila kumtukana, kumkejeli, kumtukana wala kumzushia mtu yeyote,” amesema Rais Samia na kuongeza:
“ Hata aliporudi CCM hakuwahi kwuananga kuwazodoa na kuwakebehi , wala kuwasema vibaya kule alikotoka upinzani. hapa tunapata somo kubwa sana la siasa za kujenga hoja, kuheshimiana kustahimiliana na siasa za kuleta maendeleo. Huo ndio ukomavu mkubwa wa kisiasa na njia nzuri ya kuchukua kama tunataka kumuenzi.”
Leave a comment