MWENYEKITI wa chama tawala nchini Tanzania- Chama Cha Mapinduzi (CCM) Rais Samia Suluhu Hassan, ameelekeza kutatuliwa kwa changamoto zinazoikabili Bendi ya Tanzania One Theatre (TOT). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Bendi hiyo ilianzishwa mwaka 1992 na Halmashauri Kuu ya CCM kwa lengo la kuleta hamasa ndani na nje ya Chama Cha Mapinduzi.
Jana Jumatatu, tarehe 27 Desemba 2021, Katibu wa Itikadi na Uenezi, Shaka Hamdu Shaka, aliwatembelea watumishi wa bendi hiyo yenye makazi yake Mwananyamala, jijini Dar es Salaam, akisema Rais Samia ameagiza kutekeleza agizo hilo.
Alisema, chama kitatua changamoto kadhaa zinazoikabili bendi hiyo ambazo ya namna moja zinachangia kukwamisha mafanikio ya utendaji wake
Shaka alisema hatua hiyo inalenga kuiimarisha TOT ili iendane na ukomavu na uimara wa CCM.
“Chama kitahakikisha TOT inamarika zaidi na kuzitatua changamoto zote zinazoikabili kwa nguvu zote ili bendi hii iendane na ukomavu na uimara wa Chama Cha Mapinduzi wakati tukiazimisha miaka 45 ya kuzaliwa CCM mwakani 2022,” alisema.
Aidha, Shaka aliwasisitiza watumishi wa TOT kujianda vyema kuelekea maadhimisho ya miaka 45 ya kuzaliwa kwa CCM, ambapo sherehe zake zitafanyika tarehe 5 Februari 2022.
Akizungumza kwa niaba ya watumishi wote wa TOT, Mkurugenzi Mkuu wa bendi hiyo, Gasper Tumaini alisema uamuzi wa Shaka kuwatembelea, kuzungumza nao na kuwasikiliza umewajengea ari na matumaini makubwa juu ya kuimarishwa zaidi kwa bendi yao na kutekeleza majukumu yao katika mazingira mazuri zaidi kama ilivyokua dhamira ya kuanzishwa kwake.
Tumaini alimwomba Shaka kufikisha salamu za TOT za mshikamano kwa Mwenyekiti wa CCM, Rais Samia ya kwamba wanaridhishwa na namna anayoiongoza nchi, hivyo wapo pamoja naye.
Tarehe Februari 5, mwaka 2022 CCM, itaadhimisha miaka 45 tangu kuanzishwa kwake 5 Februari 1975 baada ya kuunganishwa kwa vyama vya ASP na TANU.
Awali, akitangaza maadhimisho hayo mapema mwezi huu, Shaka alisema yatakuwa ya aina yake yakipambwa na matukio mbalimbali.
Leave a comment