RAIS wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Dk. Hussein Ali Mwinyi, ameziomba Asasi za Kiraia na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGO’s), ziunge mkono juhudi za Serikali yake katika kukabiliana na vitendo vya ukatili wa kijinsia. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
Rais Mwinyi ametoa wito huo leo Jumatano, tarehe 28 Julai 2021, akizindua mfumo wa kanzi data ya kukusanya takwimu za vitendo vya ukatili wa kijinsia, visiwani Zanzibar.
Mwenyekiti huyo wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar, amesema Serikali yake inahitaji mchango wa wadau katika kukabiliana na vitendo hivyo, ambavyo vimeshamiri visiwani humo katika siku za hivi karibuni.
“Suala hili la udhalilishaji wa wanawake na watoto linawagusa wadau wengi. Zipo taasisi za serikali zinahusika nalo lakini pia zipo taasisi binafsi. Tunahitaji nguvu ya pamoja sote kukabiliana na hili,” amesema Rais Mwinyi.
Uzinduzi wa mfumo huo umeenda sambamba na kongamano la harakati za kutokomeza vitendo vya udhalilishaji Zanzibar, lililohudhuriwa na wadau mbalimbali wa kutetea haki za binadamu.
Akizungumza katika kongamano hilo, Afisa Mtendaji Mkuu wa Shirika la Legal Services Facility (LSF), nchini Tanzania, Lulu Ng’wanakilala ameiomba Serikali ya Zanzibar, iweke mikakati ya kutokomeza vitendo vya ukatili wa kijinsia, ikiwemo mijadala na makongamano kwa kushirikisha wadau wa maendeleo ya jamii visiwani humo.
Ng’wanakilala ameiomba Serikali hiyo, pamoja na wadau wa kutetea haki za binadamu, watumie fursa ya kongamano hilo, kupata muarobaini wa vitendo vya ukatili wa kijinsia, vinavyoongoza kuathiri kuwanawake.
“Kongamano hili liwe fursa kwa wadau, katika kuweka mikakati thabiti dhidi ya ukatili wa kijinsia,” amesema Ng’wanakilala.
Mtendaji huyo wa LSF amesema, kumekuwa na vitendo vya ukatili wa kijinsia, hasa kwa wanawake na watoto.
“Ripoti yetu inaonyesha katika kila matukio manne ya ukatili yaliyoripotiwa na wanawake yalihusisha unyanyasaji wa kijinsia, ambapo visa vyote vilivyoripotiwa vinakadiriwa kufikia asilimia 26.5 kwa mwaka 2020,”
“Hii inaonesha changamoto kubwa ya upatikanaji haki, hasa kwa wanawake wanaokutana na ukatili kwenye shughuli za uchumi na nyumbani,” amesema Ng’wanakilala.
Ng’wanakilala amesema, LSF itaendelea kushirikiana na Serikali na wadau wengine wa kutetea haki za binadamu, ili kulinda haki za wanawake na makundi maalumu, yanayoongoza kwa kukabiliana na vitendo vya ukatili wa kijinsia.
“LSF kama mdau katika sekta ya upatikanaji haki na msaada wa kisheria, tutaendelea na ushirikiano na kuwa tunaamini katika nguvu ya pamoja kwenye kujenga mazingira rafiki kwa wanawake wote na kutetea kundi la watoto,” ameongeza Ng’wanakilala.
Kwa upande wa Mkurugenzi wa Jumuiya ya Wanawake Wanasheria Zanzibar (ZAFELA), Jamila Mahmoud Juma, amesema hali ya vitendo vya udhalilishaji katika jamii bado ipo kwa kiasi kikubwa, ikilinganishwa na zamani licha ya jitihada mbalimbali kufanyika.
“Tumegundua kuwa ili kuwasaidia wanawake wasidhalilike ni lazima wawezeshwe kiuchumi. Hivyo sisi kama ZAFELA tunatoa mafunzo ya uwezeshaji kiuchumi kwa wanawake ili waweze kujitegemea. Vilevile, tunatoa elimu na msaada wa kisheria kwa wanawake wanakumbana na vitendo vya udhalilishaji,” amesema Jamila.
Leave a comment