RAIS wa Zanzibar, amefanya uteuzi wa viongozi nane katika taasisi mbalimbali za umma, ikiwemo Tume ya Mipango visiwani humo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar…(endelea).
Taarifa ya uteuzi huo imetolewa leo Jumatano, tarehe 14 Desemba 2022 na Katibu Mkuu Kiongozi Zanzibar, Mhandisi Zena Said.
Taarifa ya Mhandisi Zena imewataja viongozi wapya walioteuliwa katika Tume ya Mipango Zanzibar, ambao ni Dk. Ameir Haji Sheha, aliyeteuliwa kuwa Kamishna wa Idara ya Ukuzaji Uchumi. Dk. Ameir aliwahi kuwa Mkurugenzi wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi katika Ofisi ya Rais, Kazi, Uchumi na Uwekezaji.
Kiongozi mwingine aliyeteuliwa na Rais Mwinyi, ni aliyekuwa Meneja wa Pensheni katika Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF), Mohamed Masoud Salim, ambaye ameteuliwa kuwa Kamishna wa Idara ya Mipango ya Kitaifa, Maendeleo ya Kisekta na Kupunguza Umsikini.
Naye Dk. Rukkaya Wakif Mohammed, ameteuliwa kuwa Kamisha wa Idara ya Mipango na Maendeleo ya Watendakazi. Kabla ya uteuzi huo alikuwa Kaimu Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Zanzibar (ZU).
Katika hatua nyingine, Rais Mwinyi amemteua Zainab Khamis Kibwana, kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Uratibu katika Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Idara Maalum za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ).
Rais Mwinyi amemteua Zahor Salum Elkharous, kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Uratibu wa Uchumi wa Buluu Zanzibar.
Kwenye Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Rais Mwinyi amewateua viongozi watatu, ambao ni Bihindi Nassor Khatib, aliyeteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Mipango, Sera na Utafiti.
Wakati Sitti Abass Ali, akiteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Jinsia na Maendeleo ya Jamii, huku Hassan Ibrahim Suleiman, akiteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Ustawi wa Jamii na Wazee.
“Uteuzi huo unaanzia leo tarehe 14 Desemba 2022,” imesema taarifa ya Mhandisi Zena.
Leave a comment