INSPEKTA Jenerali wa Jeshi la Polisi Tanzania (IGP), Camillus Wambura amesema katika kipindi cha kuanzia Januari hadi Oktoba 2022, matukio ya ukatili wa kijinsia 23,739 yaliripotiwa, huku 9,537 yakihusu watoto. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Slaam…(endelea).
IGP Wambura ametoa takwimu hizo jana tarehe 13 Desemba 2022, akifungua mafunzo ya siku tatu ya watendaji wa Dawati la Jinsia na Watoto, yanayofanyika jijini Tanga.
Amesema, idadi ya matukio hayo imepungua kwa visa 1,840 (asilimia 3.73), kutoka 25,579 yaliyoripotiwa kuanzia Januari hadi Oktoba 2021, hadi kufikia 23,739 kipindi kama hicho kwa mwaka huu.
“Takwimu zinaonyesha katika kipindi hicho jumla ya watu 23,739 walifanyiwa ukatili wa kijinsia ikilinganishwa na watu 25,579 kwa kipindi cha Januari hadi Oktoba 2021. Huu ni upungufu wa watu 1,840 sawa na asilimia 3.73. Ambapo matukio ya ukatili kwa watoto pekee yaliyoripotiwa 2022 ni 9,537, ikilinganishwa na kipindi kama hicho 2021 yaliripotiwa 9,789 sawa na upungufu wa matukio 252,” amesema IGP Wambura.
Mkuu huyo wa Jeshi la Polisi nchini, amesema licha matukio hayo kupungua kwa asilimia 3.73, lakini bado kazi ipo ya kuhakikisha yanatokomezwa.
“Kwa kutumia takwimu zinadhihirisha bado iko kazi na kazi hii ni kubwa mbeleni ya kufanya, ni matumaini yangu kupitia kikao hiki cha kimkakati mtaenda kuwa chachu kwa kufanyia kazi mipango mliyojiwekea kwa 2023, kuhakikisha vitendo hivi kwenye maeneo yenu ya kazi vinapungua kama sio kuisha. Hali hii itafanya jeshi kuwa kimbilio vitendo vya ukatili vinapojitokeza,” amesema IGP Wambura.
Leave a comment