KIONGOZI wa upinzani nchini Kenya, Raila Odinga, amewataka wabunge wa Umoja wa Azimio, wanaotaka kuiunga mkono Serikali ya Rais William Ruto, wajiuzulu nyadhifa zao kwa kuwa nafasi hizo walizipata baada ya wafuasi wa umoja huo kuwachagua. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Odinga ametoa kauli hiyo leo tarehe 12 Julai 2023, akitoa tamko la umoja huo kuhusu maandamano yanayoendelea Kenya.
Hii ni mara ya pili kwa mwanasiasa huyo wa upinzani kutuhumu Serikali ya Ruto kuwachukua wabunge hao, ambapo alitahadharisha kwamba nguvu ya Azimio inatokana na wananchi na sio wabunge.
“Tunaheshimu haki ya wakenya waliamua kwenye uchaguzi. Wabunge waliochaguliwa kupitia Azimio kama wanataka kuvuka mpaka waende eneo lingine wafuate sheria inavyotaka kujiuzulu. Vilevile vyama vya Azimio, Jubilee Party wakateua viongozi wapya waache kuingia ndani kuleta uamuzi bandia kuinyakua Jubilee, hayo mambo yanaweza leta maafa katika nchi yetu,” amesema Raila.
Raila amesema “wabunge wa Jubilee wanataka kuvuka mipaka sababu ya umalaya wa siasa, waende lakini waache chama cha Jubilee ndani ya Azimio.”
Akizungumzia maandamano yanayofanyika ambayo hadi sasa yamesababisha kifo cha mtu mmoja aliyepoteza maisha kufuatia majeraha ya risasi za Polisi, Raila amesema yataendelea hadi pale Rais Ruto atakaposikiliza kilio cha wananchi kwa kurekebisha Sheria ya Fedha inayolalamikiwa kwamba imeongeza gharama za maisha.
“Wakenya wamechoka kwa ahadi, kuambiwa nini cha kufanya na nini si cha kufanya. Watu wamechoka kusikia njaa, wazazi wamechoka kurudi nyumbani bila kitu baada ya harakati za siku nzima, kuchukuliwa fedha zao wanazotafuta na Serikali kwa kigezo cha kodi,” amesema Raila.
Jeshi la Polisi nchini Kenya, limepiga marufuku maandamano hayo, huku likiwatawanya wafuasi waliokuwa kwenye uwanja wa Kamukunji jijini Nairobi, kusubiri hotuba ya Raila, kwa mabomu ya machozi.
Leave a comment