MFUKO wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umeweka wazi kuwa kitendo cha waajiri kuchelewesha michango ya watumishi kinasababisha tozo ya ucheleweshaji wakati wa kulipa mafao kwa wanachama. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza jana tarehe 6 Novemba 2022, jijini Dar es Salaam, wakati wa Mkutano Mkuu wa Klabu ya Waandishi wa Habari Dar es Salaam (DCPC), Meneja wa PSSSF Temeke, Rajabu Kinande amesema kitendo cha mwajiri kuchelewesha mchango huo kunaathiri mafao ya mwanachama.
“Ili kupunguza malalamiko ni vyema waajiri kutimiza wajibu wao kisheria wa kulipa michango ya watumishi wake ndani ya mwezi mmoja baada ya mwisho wa mwezi husika” alisema Kinande.
Kinande alisema utaratibu wa kufanya malipo upo kiteknolojia ambapo kumbukumbu za malipo zitahifadhiwa.
“Kwa sasa mwajiri ana uwezo wa kutengeneza namba za kumbukumbu ya malipo itakayomuwezesha kulipa michango na kupata risiti kupitia mtandao,” alieleza.
Wakati huo huo Kinande alisema wastaafu wengi wanachelewa kupata mafao yao kutokana na kuchelewesha taarifa zao za kustaafu kabla ya miezi sita.
Aidha, alisema kuwa hakuna watumishi wanaowafanyia mpango wastaafu wengine kupata mafao mapema badala yake uwahishaji wa taarifa zao ndio unawasaidia kupata stahiki zao haraka.
Alisema baada ya kupata taarifa hiyo, mtumishi anatakiwa kuanza kufuatilia mafao yake kwa kupeleka taarifa zote muhimu katika ofisi hizo ili zianze kufanyiwa kazi ikiwemo kufuatilia kama waajiri wamechangia miezi yote kama inavyotakiwa na sheria.
Alisema kila mwaka mfuko huo hufanya uhakiki wa wastaafu na wategemezi wanaopata pensheni kwa lengo la kusafisha daftari la wastaafu na kuhakikisha pensheni inalipwa kwa walengwa na si vinginevyo.
Leave a comment