KWA mara ya kwanza sasa wakulima, wavuvi na wafugaji nchini Tanzania wanaweza kupata mikopo kutoka Benki ya NMB kwa ajili ya kuendeleza shughuli zao kwa riba nafuu, baada ya taasisi hiyo kupunguza riba hadi asilimia 9. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Hatua ya benki hiyo kupunguza riba ni utekelezaji wa maagizo ya Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan aliyotoa mwaka huu kwa taasisi za kifedha kupunguza riba hadi kufikia namba moja.
Oscar Nyirenda, Kaimu Ofisa Mkuu Udhibiti na Utekelezaji wa NMB mwishoni mwa wiki iliyopita akizungumza katika warsha ya wafanyabiashara wadogo na wa kati wa benki hiyo, (Business club) katika mikoa ya Lindi na Mtwara alisema benki hiyo imepunguza riba ya mikopo kwa sekta mama za kilimo, uvuvi na ufugaji hadi kufikia asilimia 9 mwaka 2022.
Mbali na hilo alisema, benki hiyo imeendelea kushusha riba kwa wateja wadogo wanaokopa kuanzia Sh 500,000 hadi millioni tano kulingana na maombi na vigezo vya mkopaji.
Alisema hatua hiyo ilikuja kufuatia ushauri kutoka kwa Rais Samia Suluhu Hassan aliyezitaka benki nchini kupunguza riba hadi kufikia namba moja, (Single digit).
“Sisi kabla ya ushauri wa Mheshimwia Rais tulipunguza hadi asilimia 10 lakini baada ya ushauri mwezi Mei mwaka huu tumepunguza hadi asilimia 9 kwa sekta tatu mama,” alisema Nyirenda.
Alisema kuanzia Julai, 2021 hadi Juni 2022 mikopo 37,500 yenye thamani ya Sh 752.7 Bilioni imetolewa kwa wafanyabiashara wadogo na wa kati kwa ajili ya kuendeleza shughuli zao za biashara.
Alisema kushuka kwa riba imesababisha idadi ya wafanyabiashara wanaokopa katika benki hiyo kuongezeka kulinganisha na miaka ya nyuma kabla ya NMB kupunguza kwa kiwango hicho cha riba ya mikopo yake.
“Sote tunajua kwamba riba ni bei ya bidhaa kama bidhaa nyingine kwa hiyo kubadilisha bei hizo kunahitaji maamuzi thabiti ambayo yatakuwa amzuri na kuleta matokeo chanya”
Meneja wa NMB Kanda ya kusini, Janeth Shango alisema benki hiyo iko tayari kuwahudumia wafanyabiashara katika mitaji na elimu ili huduma zao ziwe na ufanisi na faida kwao pia.
Alisema benki hiyo hutoa mikopo kwa wafanyabiashara wadogo,wakubwa na wa kati kulingana na biashara ya mteja na uhitaji unaendana na biashara tajwa.
Mwenyekiti wa klabu ya wafanyabiashara ya benki hiyo mkoa wa Mtwara, Hamisi Bandari alisema changamoto walizonazo ni pamoja na kutokuwa na elimu masuala ya kodi, utunzaji na usimamizi wa fedha na hofu ya kutafuta mitaji.
Aliwataka wafanyabaishara wa Mtwara kujipanga kuchangamkia fursa za kibiashara zinazofunguka hususani za visiwa vya Comoro na wenye mitaji midogo kufika benki ya NMB kuomba mikopo.
Mwenyekiti wa Wafanyabiashara wa Mkoa wa Lindi, Hamis Livembe akaiomba serikali pamoja na taasisi za kifedha kuwatengenezea mazingira mazuri ya kifedha ili waweze kushiriki katika miradi mikubwa iliyopo mkoani humo
Alisema uwapo wa Sh trilioni 70 katika mradi mkubwa wa gesi LNG unaashiria mabadiliko makubwa ya kimaendeleo mkoani Lindi kwani wajasiriamali na wafanyabiashara kunufaika na mradi huo hapo baadae.
Lakini walisema bila serikali na taasisi za kifedha kuwapatia mikopo nafuu na mazingira thabiti ya wao kuweza kuwafikia watu wengi wanaokadiriwa kufika mkoani humno miradi hiyo haitakuwa na maana kwao….
Leave a comment