BENKI ya NMB imetangaza dhamira yake ya kutoa masuluhisho thabiti ya kifedha kwa Wafanyabiashara Wakubwa, Kati na wa Wadogo (MSMEs) ili kuwawezesha kuchangamkia fursa zilizopo kwenye Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA). Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Hayo yalisemwa na Mkuu wa Kitengo cha Miamala wa Benki ya NMB, Linda Teggisa wakati akitoa mada kwenye mdahalo wakati wa mkutano wa AfCFTA wa wanawake katika biashara uliyofanyika jijini Dar es Salaam jana.
Akizungumza wakati wa mdahalo huo, Teggisa alisema fedha zitakazotolewa na benki hiyo zitakuwa katika mfumo wa mikopo ya mitaji na mikopo ya rasilimali, kwa lengo la kuwawezesha wafanyabiashara hao kukuza mitaji yao iliwaweze kushindana kikamilifu katika kufanya biashara barani Afrika.
Alisema benki yake kwa kuzingatia utendakazi wake thabiti na mizania itatoa mikopo kwa wajasiriamali wanaostahili kama sehemu ya dhamira yake ya kuwezesha biashara za ndani kushindana kikamilifu katika bara la Afrika.
“Kama benki, tumepata mafanikio makubwa sana kiutendaji mwaka huu na hivyo kutufanya kuwa benki ya tatu iliyopata faida kubwa kwenye jumuiya yaAfrika Mashariki mwaka huu. Vilevile, benki yetu imekuwa nambari moja kwa kuzingatia mtaji wa soko.
“Hayo yote yanaonyesha kuwa benki yetu inaendelea kuwa imara siku had siku na huduma tunazozitoa zinalenga sehemu mbalimbali za wateja wa rejareja na wa jumla,” Teggisa alisema.
Akizungumzia mada ya ‘Wanawake katika Biashara’, Teggisa alisema kuwa benki yake inatambua kuwa wanawake wengi wanajishughulisha na biashara ndogondogo hivyo wanapaswa kujengewa uwezo katika biashara wanazoanzisha ili ziweze kukua.
“Kwa misingi hiyo, wanahitaji washirika kama Benki ya NMB kuwasaidia katika safari hii. Kama benki, kwa makusudi tulianzisha bidha maalum ya wanawake lililopewa jina la ‘Jasiri’ kama sehemu ya juhudi zetu za kuhakikisha ustawi na uendelevu wa biashara zinazomilikiwa na wanawake,” aliongeza.
Teggisa alibainisha kuwa benki yake pia imeendelea kuwekeza katika teknolojia hali ambayo imewezesha benki hiyo kutoa suluhu za malipo ya kidijitali kwa wateja wake kote nchini kama sehemu ya mkakati wake kabambe wa kuharakisha ujumuishaji wa kifedha.
“Tuna masuluhisho mengi ya kidijitali ambayo yanapatikana kupitia app yetu ya simu na mfumo wa USSD. Pia tunayo huduma ya mikopo midogo inayoitwa ‘Mshiko Fasta’ ambayo inamwezesha mtu kupata mkopo wa papo kwa papo ya hadi shilingi elfu 50 (500,000).
Teggisa wakati wa hafla hiyo aliwataka wanawake kushirikiana na kuunda vikundi huku akisisitiza kuwa hatua hiyo itasaidia kuongeza ushindani ao kwenye Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA).
Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA) ni utaratibu wa pamoja wa nchi wanachama wa Umoja wa Afrika unaolenga kuchochea uchumi na Biashara miongoni mwa nchi wanachama.
Lengo hilo litafikiwa kwa kufunguliana masoko ya biashara ya bidhaa na huduma kwa kuondoleana ushuru wa forodha (tariff) na kulegezeana masharti na taratibu nyingine zisizokuwa za kiushuru.
Dhamira yake kuchochea ukuaji wa uchumi na biashara baina ya nchi wanachama (intra-Africa trade) kwa dola za kimarekani trilioni 29 ifikapo mwaka 2050.
Leave a comment