MGOMBEA nafasi ya Mwenyekiti wa Klabu ya Simba, Juma Nkamia amesema, akipewa ridhaa ya uongozi ndani ya klabu hiyo atahakikisha anasimama na asilimia 51 za wanachama kwenye bodi ya wakurugenzi, sambamba na kushirikiana na mwekezaji Mohamed Dewji mwenye hisa asilimia 49. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Nkamia ameyasema hayo wakati akijinadi mbele ya wanachama waliohudhulia Mkutano Mkuu unaofanyika leo tarehe 7 Februari 2021, kwenye ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere huku moja ya ajenda yake ikiwa ni uchaguzi mdogo wa kuziba nafasi ya mwenyekiti iliyoacha wazi na Swedy Nkwabi mara baada ya kujiuzuru.
Pamoja na mengineyo Nkamia amesema kuwa atasimama upande wa wanachama ambao wanamiliki hisa asilimia 51 kwenye bodi hiyo kwa lengo la kuleta umoja na kutoa elimu kwa wale wote wapinga mabadiliko.
“Mkinipa nafasi kazi yangu kusimamia 51% ya wanachama wa Simba na nitashirikiana kwa dhati na mwekezaji, Dewji pamoja na wajumbe wote wa bodi,” alisema Nkamia.
Mgombea huyo aliendelea kusema kuwa atajitahidi kuwapa elimu wale wanachama wa klabu hiyo ambao ni wapinga mabadiliko ya uwendeshaji wa timu kwa mfumo wa kisasa.
“Moja ya lengo langu ni kuleta umoja hata wanaopinga mabadiliko tukae nao tuwafundishe,” aliongezea mgombea huyo.
Ikumbukwe Nkamia alishawahi kuwa Mbunge wa bunge la jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwakilisha jimbo la Nchemba kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM).
Leave a comment