MTANDAO wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), umeyataka Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGO’s), kuendelea kuzingatia matakwa ya kisheria ili kukwepa hatari ya kufutiwa usajili wake na Serikali. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Tamko hilo limetolewa leo tarehe 3 Machi 2023 na Kaimu Mratibu Taifa wa THRDC, Nuru Maro, baada ya Msajili wa NGO’s kutoa notisi ya kutaka kuyafuta mashirika mengine 2,915.
Ni baada ya kufuta mengine 4,897, yaliyofanya makosa mbalimbali ikiwemo kutowasilisha taarifa zao zaidi ya miaka miwili, pamoja na kushindwa kulipa ada.
“THRDC inatoa wito kwa mashirika kuendelea kuzingatia matakwa ya kisheria na kikanuni kwa sasa ili kuepuka kuingia kwenye hatari ya kusimamishwa kufanya kazi au kufutwa kabjsa. Pia, kuendelea kushirikiana na Serikali katika kufanya kazi ili kuleta maendeleo ya jamii, kiuchumi na utamaduni,” limesema tamko hilo.
Tamko hilo limeonyesha kuwa, baadhi ya mashirika yaliyohatarini kufutwa yanakabiliwa na makosa ya kutolipa ada, changamoto inayosababishwa na ukosefu wa wafadhili, ambapo amezitaka kutafuta njia mbadala za upatikanaji fedha kwa kuwekeza katika biashara mbalimbali.
Aidha, THRDC umezitaka NGO’s kutoa taarifa kwa maandishi kuhusu shirika ambalo linafanya kazi kwa kujitolea lakini halina ada za mwaka, huku akiwataka wafadhili na wadau wa maendeleo kuendelea kuyafadhili.
Katika hatua nyingine, THRDC umelitaka Baraza la NGO’s (NACoNGO) na Ofisi ya Msajili wa mashirika hayo, kufanya utafiti ili kubaini changamoto zinazopelekea zishindwe kufuata Sheria.
Leave a comment