MKURUGENZI Mkuu wa Baraza la Taifa la Uhifadhi wa Mazingira (NEMC), Dk. Samuel Gwamaka ameitaka miradi ya maendeleo inayoanzishwa iwe inazingatia uhifadhi wa mazingira pasipo kubugudhi wananchi. Anaripoti Eliabu Kanyika, DSJ … (endelea).
Dk. Gwamaka amesema hayo alipokutana na vyombo vya habari leo tarehe 3 Machi 2023 mkoani Dodoma akiitaka miradi inayoaanza iwe na tathmini ya athari kwa jamii kwa kuzingatia sheria na kanuni za mazingira.
Amesema, ili mradi uwe na maendeleo kwa jamii lazima uwe na tathmini ya athari na faida kwa jamii.
“Kabla hujaanza kujenga mradi wako cha kwanza tunachojiuliza huo mradi utaleta faida gani na unaweza ukasababisha athari gani za kijamii na kiafya kwenye jamii,” amesema Dk. Gwamaka.
Pia amesema miradi inayoanza bila ya kuwa na tathmini ya athari ya mazingira imepelekea kero na uharibifu kwa jamii.
Sambamba na hilo amezungumzia usimamizi wa hifadhi ya mazingira kwa kuzingati masharti yaliyopo katika sheria ya mazingira yanatekelezwa ipasavyo.
Amesema baraza hilo lina majukumu ya kutoa amri mbalimbali za kuzuia shughuli zinazoharibu au zenye muelekeo wa kuhatarisha mazingira au afya ya jamii.
Katika mojawapo ya majukumu ambayo Dk. Gwamaka ameyazungumzia katika mkutano huo, amesema baraza hilo lina majukumu ya kutoa elimu ya mazingira kwa jamii.
“Pamoja na kufanya na kuratibu tafiti zinazohusu maswala ya kimazingira kuna maeneo mengi sana ambayo bado ni changamoto, basi baraza lina jukumu hilo la kuendelea kuelimisha umma,” amesema Gwamaka.
Katika kujumuisha Dk. Gwamaka amesema baraza hilo limeweza kupata mafanikio mbalimbali ikiwa ni sera mpya ya mazingira ya mwaka 2021, na kwamba kabla ya kuanzishwa kwa sera hiyo kulikuwa na changamoto nyingi hususani mabadiliko ya tabia ya nchi na ongezeko la matumizi ya kemikali viwandani.
Na pia amesema kwamba huduma kwa wateja zimeboreshwa katika kuendeleza maendeleo ya baraza hilo la mazingira.
“Sasa hivi mtu huna haja ya kwenda kwenye ofisi za NEMC kufanya usajili wa tathmini athari za mazingira kwa jamii, kuna mifumo ambayo ukiingia kwenye mtandao unapata majibu yote kutokea pale,” amesema Dk. Gwamaka.
Leave a comment