BENKI ya Taifa ya Biashara (NBC) imeandaa hafla ya futari kwa ajili ya wateja wake visiwani Zanzibar, huku Spika wa Baraza la Wawakilishi, Zubeir Ali Maulid akiipongeza benki hiyo kutokana na ushirikiano inaoutoa katika nyanja mbalimbali ikiwemo kijamii na kiuchumi. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Akizungumza kwenye hafla hiyo iliyofanyika jana tarehe 9 Aprili, 2022 Visiwani Zanzibar, Spika Zubeir alionyesha kuridhishwa na namna benki hiyo inavyoshirikiana na Baraza hilo pamoja na serikali katika kuleta maendeleo visiwani Zanzibar kupitia mipango yake mbalimbali ikiwemo ile inayogusa moja kwa moja ustawi wa jamii pamoja na serikali.
“Pamoja na yote hayo zaidi niwapongeze NBC kwa kuonesha umuhimu wa wateja wake kwa kurejesha miongoni mwa faida wanazozipata kwa namna mbalimbali ikiwemo ikiwemo kwa njia hii ya kufutarisha na kutoa huduma nyengine mbali mbali kwa jamii…tunashukuru,’’ alisema.
Awali akizungumza katika hafla hiyo ya futari, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC, Theobald Sabi alisema benki hiyo imeamua kuandaa futari hiyo ili kujumuika na wateja wake kama hatua ya kuonyesha mshikamano na umoja katika kipindi cha mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Alisema benki hiyo inaheshimu sana Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kutokana na ukweli kwamba, ni kipindi ambacho mwanadamu anajiweka karibu na Muumba wake kupitia mfungo na kufanya maombi.
“Huu ni mwezi ambao pia unatukumbusha kufanya kilicho chema mbele za Mungu wetu. Kwa kuwa NBC siku zote tupo karibu imani za wateja wetu tumeamua kuandaa futari hii ili kujumuika na wenzetu kufanikisha hilo,” amesema Sabi.
Zaidi alibainisha kuwa benki hiyo ina huduma maalum inayojikita katika kutoa huduma kwa wateja wake wa imani ya Kiislam, ijulikanayo kama Islamic Banking inayopatikana kwenye matawi yote ya benki hiyo ikiendeshwa katika misingi ya dini hiyo ikiwa na huduma mbalimbali ikiwemo mikopo ya riba.
Sabi aliwaomba wale ambao hawajajiunga na benki hiyo kufungua akaunti zao ili waweze kufurahia huduma bora na za kipekee zinazotolewa katika matawi yote ya NBC nchini.
Hafla hiyo ya futari ilihudhuriwa na wageni mbalimbali wakiwemo mawaziri, viongozi wa dini, viongozi wa vyama vya siasa, wateja, mawakala pamoja na wafanyakazi wa benki hiyo.
Leave a comment