RAIS Mstaafu Jakaya Kikwete amesema atamkumbuka Hayati Ali Hassan Mwinyi kwa kuwa kiongozi msikivu na mwenye maamuzi magumu. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Amesema wakati akiwa Serikali, Mwinyi aliyekuwa rais wa awamu ya pili alivunja baraza la mawaziri mara mbili.
Akizungumza katika shughuli ya kuaga mwili wa Hayati Mzee Mwinyi zilizofanyika leo Ijumaa katika uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam, Kikwete amesema mara ya kwanza aliwaitwa mawaziri na manaibu mawaziri na kuwaambia waandike barua za kujiuzulu.
“Alipokuja hakuonesha bashasha la kawaida, alisema tu ‘nawashukuru sana kwa mlivyonisaidia kwa miaka yote ila wenzangu naomba muende mkajiuzulu’.
“Tukatazamana wote… tukajiuzulu!, alivyosema akainuka akaondoka basi na sisi tukatoka,” amesema.
Kikwete ameendelea kusimulia kuwa baada ya kutoka ofisini kwa rais walitembea kwa miguu hadi katika ofisi za waziri wa fedha kwa kuwa magari yao hayakuwepo, walikuwa wamewaruhusu madereva kurejea ofisini.
“Namshukuru Msuya alikuwa waziri wa fedha. Alitupatia gari, baada ya muda ikaja barua kwa wote tumefukuzwa.
Iliandikwa kwamba ondokeni ofisini kakaeni nyumbani, mpaka mtakapoitwa tena. Basi lilipoundwa Baraza nikawa waziri kamili,” amesema.
Mara ya pili, Kikwete amesema ilikuwa tofauti kwa taarifa ya kuvunja baraza la mawaziri ilitangazwa kwenye vyombo vya habari.
“Alikuwa mtu jasiri hivyo watanzania wenzangu tumkumbuke mzee huyo, ndiyo kiongozi aliyefikisha nchi yetu hapa kutoka kwenye mabadiliko ya mfumo tuliokuwa nao.
“Ni mtu muungwana sana, mwema ana huruma ila dhabiti kwenye uamuzi. Na hilo ndio funzo kwa viongozi kwamba unaloliamini bora liwe na masilahi kwa taifa, likomalie,” amesema.
Leave a comment