KAMPUNI ya Usafirishaji majini, PMM Shipping Limited imezindua huduma ya kusafirisha makontena kutoka Bandari ya Dar es Salaam, kwenda maeneo mengine ikiwemo visiwa vya Comoro, Mombasa nchini Kenya na South Afrika. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Uzinduzi huo umefanywa leo Ijumaa, tarehe 4 Agosti 2023 na Mkurugenzi wa Bandari ya Dar es Salaam, Mrisho Selemani Mrisho.
Mrisho amesema huduma hiyo inayotarajiwa kutolewa na meli kubwa ya Mv Mirembe Judith kwa kuwa gharama zake ni nafuu na ina uwezo mkubwa wa kubeba makasha (kontena), kwa wakati mmoja.
“Uzinduzi wa huduma ya Meli ya Mv Mirembe Judith, itasaidia wafanyabiashara wanaopeleka mizigo yao Zanzibar, sababu awali walikuwa wanapata shida ya kutumia meli ndogo lakini meli hii kubwa iliyokuja leo itasaidia utatuzi wa changamoto za usafirishaji makasha,” amesema Mrisho.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkurugenzi wa Masoko wa Kampuni ya PMM Shipping Limited, Deogratius Chacha amesema nia yao ni kupanua huduma hiyo ifikapo 2024, ambapo wanatarajiwa kuongeza meli nyingine mbili kwa ajili ya kusafirisha mafuta na bidhaa zisizochakatwa.
“Sisi kauli mbiu yetu ni kutoa huduma ya uhakika katika usafiri wa majini na tumeanza na meli hii (MV Mirembe Judith) na hatuishii hapa hadi 2024 tuna meli mbili zinakuja moja ya mizigo isiyochakatwa na nyingine ya mafuta,” amesema Chacha.
Aidha, Chacha ameishukuru Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kuwawezesha wawekezaji wa ndani, akiwemo mmiliki wa Mv. Mirembe Judith.
“Tunamshukuru Rais Samia kwa jinsi anavyowezesha wawekezaji wa ndani ndiyo maana imetuwezesha kufika hapa tulipo, bila ya yeye tsuingefikia hapa tulipo. Na tunashukuru uongozi wa Bandari ya Dar es Salaam, kwa ushirikiano waliotupatia mpaka tunashusha mzigo ndani ya muda mfupi,” amesema Chacha.
Leave a comment