MUSWADA wa Bima ya Afya kwa Wote wa 2022, umewasilishwa bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu na kusomwa kwa mara ya pili, baada ya kufanyiwa marekebisho katika baadhi ya mapendekezo yake ambayo yalipingwa na wabunge pamoja wadau mbalimbali. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Muswada huo wa kutunga sheria ya bima ya afya kwa wote namba nane, umesomwa kwa mara ya pili bungeni jijini Dodoma leo tarehe 1 Novemba 2023.
Akiwasilisha muswada huo, Ummy amesema umelenga kuimarisha ustahimilivu na uhimilivu wa skimu za bima ya afya kwa kuifanya kuwa ya lazima, pamoja na kufikia malengo ya kufikia huduma ya afya kwa wote.
Pia, Ummy amesema Serikali inapendekeza kuanzishwa kwa mfuko wenye lengo la kugharamia bima ya afya kwa watu wasiokuwa na uwezo. Pia, itagharamia huduma za matibabu kwa magonjwa sugu na ya muda mrefu kama vile saratani, figo na huduma za dharura zinazotokana na ajali.
Amesema kwa sasa asilimia 85 ya watanzania hawana bima ya afya na kwamba takwimu zinaonyesha kuwa hadi Septemba 2023, asilimia 15.3 ya watanzania wote wapo katika mfumo wa bima ya afya.
Akitaja athari za bima ya afya kuwa sio ya lazima, Ummy amesema imepelekea asilimia kubwa ya wanaojiunga kwa hiari kuwa wagonjwa na kwamba bima hiyo inatakiwa kuwa ya kuchangiana kati ya wagonjwa na wasio wa wagonjwa.
Waziri huyo wa afya amesema ili kuongeza ushiriki wa watanzania, muswada huo unapendekeza kuwekwa adhabu ya asilimia 10 ya mchango wa kila mwaka kwa mtu ambaye hatajiunga na bima hiyo kwa kipindi cha miaka mitatu.
“ Hata hivyo, Waziri amepewa mamlaka ya kutoa msamaha wa ulipaji wa adhabu ya asilimia 10 kwa kuzingatia maslahi ya umma au sababu nyingine yoyote, tutawekeza zaidi kwenye elimu na hjamasa na tutajitahidi kuboresha huduma za afya ili wananchi wengi wavutiwe,” amesema Ummy.
Leave a comment