ALIYEKUWA Mkuu wa Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro, Lengai Ole Sabaya amefika mbele ya Mahakama ya Rufani jijini Arusha, kusikiliza rufaa iliyofunguliwa na Jamhuri dhidi yake, kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu, kumwacha huru baada ya kutengua adhabu ya kifungo cha miaka 30 jela, aliyohukumiwa kwa kosa la unyang’anyi wa kutumia silaha. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha…(endelea).
Sabaya amewasili mahakamani hapo leo Jumatano, tarehe 1 Novemba 2023, pamoja na wenzake wawili, Sylvester Nyegu na Daniel Mbura, ili kusikiliza rufaa hiyo iliyoko mbele ya jopo la majaji watatu wa Mahakama ya Rufaa.
Hatua hiyo inajiri baada ya Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), kufungua rufaa hiyo ikipinga uamuzi uliotolewa Aprili 2023 na Mahakama Kuu, mbele ya Jaji Sedekia Kisanga, wa kutengua hukumu iliyotolewa na Hakimu Odira Amoro, wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, ya kifungo cha miaka 30 jela.
Hakimu Amoro alitoa hukumu hiyo baada ya kuwakuta Sabaya na wenzake kuwa wana hatia, katika mashtaka yaliyokuwa yanawakabili kwenye kesi ya jinai Na. 105/2021.
Katika kesi hiyo, Sabaya na wenzake walikuwa wanakabiliwa na mashtaka ya unyang’anyi, wakidaiwa kuchukua kwa nguvu fedha kiasi cha Sh. 399,000 kutoka kwa Diwani wa Sombetini, Bakari Msangi. Sh. 2 milioni za mfanyabiashara na Sh. 39,000 za Ramadhan Ayub pamoja na simu yake ndogo aina ya Tekno.
Lakini Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, ilitengua adhabu hiyo baada ya Sabaya na wenzake kukata rufaa kupinga uamuzi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, wa kuwapa kifungo cha miaka 30 jela, baada ya kuwakuta na hatia katika kesi iliyokuwa inawakabili.
Miongoni mwa hoja zilizopelekea sabaya na wenzake kushinda kwenye rufaa hiyo kisha kuachwa huru baada ya kusota kifungoni kwa takribani miezi 11, ni mashahidi kupishana kwenye ushahidi wao, kupishana kwa maelezo, baadhi ya madhahidi kutohojiwa na washtakiwa.
Leave a comment