MTANZANIA aliyefahamika kwa jina Michael (Mike), anadaiwa kuuawa na rafiki yake aliyemfuata Afrika Kusini, kumdai pesa zake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Kwa mujibu wa taarifa zilizosambaa mitandaoni kuanzia juzi Jumatatu, Mike aliyekuwa anafanya biashara zake nchini Msumbiji, anadaiwa kuuawa na mtanzania mwenzake anayefahamika kwa jina la Misheli, siku chache tangu alivyomfuata jijini Johannesburg, Afrika Kusini, ili amlipe haki yake.
Inadaiwa kuwa, marehemu Mike alivyofika Afrika Kusini, alikutana na Misheli, baada ya muda mchache hakupatikana kwenye simu ambapo watanzania wenzake walianza kumtafuta.
Siku nne baada ya kumtafuta bila mafanikio, inadaiwa asubuhi ya tarehe 18 Machi 2024, mwili wake ukipatikana katika chumba cha kuhifadhia maiti katika Hospitali ya Hilbrow, jijini Johannesburg, ambapo inaonesha aliuawa kwa kupingwa risasi.
“Kutokana na taarifa za mochwari, mwili wa Mike umekutwa mtaani tarehe 11 Machi 2024,” inadai taarifa hiyo.
MwanaHALISI Online imezungumza na Balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini, James Bwana, Kwa ajili ya kuthibitisha ukweli wa tukio hilo, ambaye alikiri kuwa na taarifa zake.
Balozi Bwana alisema kwa sasa ubalozi unafuatilia ili kuthibitisha kama aliyefariki ni mtanzania kisha watatoa taarifa.
“Unajua huku watanzania wako wengi na changamoto iliyopo baadhi yao wanaishi bila vibali na passport Sasa sisi kama ubalozi tunakosa taraifa zao, hivyo ikitokea mtu amefariki inakua ngumu kuthibitisha kama ni mtanzania.
“Hadi tufanye uchunguzi kujiridhisha kama ni mtanzania na hata kama akibainika ni mtanzania kusafirisha mwili wake huko huwa inakuwa changamoto kama anakuwa hana nyaraka sababu kuna baadhi ya fomu inabidi kujaza ili mwili uweze kutolewa huku kuletwa Tanzania,” amesema Balozi Bwana na kuongeza:
“Sasa hizo taraifa ni kweli tunazo lakini hatuwezi kuzithibitisha hadi tufanye ufuatiliaji kuthibitisha kama kweli ni mtanzania sababu watu wengi wanaodaiwa kuwa watanzania wameripotiwa kufariki dunia hivi karibuni na Bado tunafuatilia kuthibitisha kama kweli ni watanzania Kisha tukijiridhisha tutatoa majina yao.”
Leave a comment