CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema kinajiandaa kushiriki chaguzi zijazo, huku kikiweka wazi kuwa, kitatoa msimamo mzito ifikapo Januari 2024, iwapo Serikali haitafanyia kazi mapendekezo yao juu ya marekebisho ya sheria za uchaguzi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Kauli hiyo ilitolewa jana Jumatano na Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika, akiwa ziarani nchini Marekani, wakati anahojiwa na Idhaa ya Kiswahili ya Sauti ya Amerika (VOA).
Ikumbukwe kuwa, Chadema kiliweka msimamo wa kutoshiriki chaguzi zozote endapo marekebisho ya sheria za uchaguzi pamoja na maeneo ya kiuchaguzi katika katiba ya 1977, hayatafanyika.
“… Tumejiandaa kwa mazingira ya mbele sababu kuna chaguzi na tunajiandaa hatusubiri tupate marekebisho. Nini tutafanya, tutawaongoza namna gani wananchi kama marekebisho hayajafanyika, tutatoa maelekezo Januari,” alisema Mnyika.
Kabla ya Mnyika kutoa kauli hiyo, aliilaumu Serikali akidai imepuuza mapendekezo yaliyotolewa na Chadema , kwa ajili ya marekebisho ya sheria za uchaguzi.
Ametaja mapendekezo ambayo alidai Serikali haijayafanyia kazi kuwa ni pamoja na, matokeo ya uchaguzi wa rais kuhojiwa mahakamani, maamuzi ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuhojiwa mahakamani katika hatua yoyote ya kiuchaguzi. Upatikanaji wa tume huru ya uchaguzi na mgombea binafsi.
“Kitu ambacho wameweka kwenye sheria inayopendekezwa ni kamati ya usaili , lakini haihusiki kwenye usahili wa mwenyeti , makamu mwenyekiti na mkurugenzi wa tume. Inahusu wajumbe tu, sisi tulisema kuanzia kwenye katiba tuondoe utaratibu wa rais kuteua mwenyekiti, makamu na mkurugenzi,” alisema Mnyika.
Leave a comment