RAIS Samia Suluhu Hassan amesema Serikali inakwenda kuunganisha mafunzo ya vitendo kwa vijana kupitia mpango wa “Jenga Kesho Iliyobora” Building Better Tomorrow (BBT) pamoja na mafunzo yanayotolewa na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) ili vijana watakaohitimu mafunzo ya jeshi hilo wawe na muelekeo. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo tarehe 10 Julai 2023 wakati akihutubia kilele cha miaka 60 ya JKT katika uwanja wa Jamhuri Dodoma.
Ameiagiza wizara ya ulinzi kukarabati makambi hayo ya jeshi ili kutekeleza mpango huo haraka.
“Tunaposema tunakwenda kukarabati makambi zaidi, yanayokwenda kurekebishwa mbali na mafunzo ya ukakamavu na kijeshi yatakwenda yataungana na mpango wa BBT ili kuwajengea kesho nzuri vijana. Wanapotoka wajue wanakwenda wapi kufanya nini kinyume na sasa wanazubaa mitaani.
Aidha, amesema anatamani kuona JKT linakuwa la kisasa lenye kuwalea vijana katika uzalendo.
Amesema vijana wanaotoka JKT wanapaswa kuwa wazalendo katika nchi yao na hata wanaobaki katika majeshi na vyombo vya ulinzi wawe watu wenye weledi wa kupigiwa mfano.
“Katika miradi mikubwa mmefanya vizuri sana ikiwemo ujenzi wa Ikulu ya Chamwino, sisi Serikali tutaendelea kuwaunga mkono na ikibidi mpate mikopo ili kuongeza nguvu ya uzalishaji tuko tayari kuwadhamini,” amesema Rais Samia.
Amesema vijana wanaopita JKT wanapaswa kubeba dhima ya uzalendo mioyoni mwao siyo katika midomo kwani jeshi linawafanya vijana kuwa wamoja na wenye kuithamini nchi yao katika kuonyesha uzalendo.
Amesema idadi ya vijana waliokwenda JKT kwa mujibu wa sheria ni 52,000 ikiwa ni ongezeko kubwa kutoka 30,000 walioitwa mwaka jana baada ya kumaliza kidato cha sita.
Leave a comment