MBUNGE wa Jimbo la Kilosa Prof. Palamagamba Kabudi amefanya ukaguzi wa ujenzi wa Tuta la kuzuia maji yanayotapika nje ya Mto Mkundi uliopo kata ya Dumila Wilayani Kilosa na kusababisha mafuriko katika makazi ya watu wanaoishi pembezoni mwa mto huo na kusababisha athari za uhalibifu wa mali na kuhatarisha Maisha ya wakazi wa maeneo hayo. Anaripoti Yusuph Kayanda, Morogoro … (endelea).
Akiongozana na Diwani wa kata ya Dumila Deuglas Mwigumila, Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi katika kata Saburi Sabuni, Mratibu wa shughuli za Jimbo Everist Msakila na wajumbe wa kamati ya Ulinzi na usalama kata hiyo Prof, Palamagamba Kabudi amewasisitiza wananchi wanaoishi pembezoni mwa mto huo kuacha kufanya shughuli za kilimo pembezoni mwa mto huo ili kuzuia uharibifu unasababisha mto huo kutoroka katika mkondo wake.
Ujenzi wa kujenga tuta hilo la udongo pamoja na juhudi za kuchimbua mto Mkundi ulitokana na athari za Mvua kubwa zinazoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali hapa Nchini na kusababisha mafuriko katika maeneo ya makazi ya watu hali iliyosababisha uharibifu wa mali pamoja kuhatarisha usalama wa wananchi.
Aidha Prof, Kabudi alitoa shukrani za dhati kwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa hatua Madhubuti alizochukua kwa wakazi wa Kilosa waliokumbwa na mafuriko katika kata za Kidete, Mamboya, Dumila kutokana na mto huu Mkundi, Msowero, Mvumi, Rudewa, Mkwatani, Kimamba ‘A’ Tunamshukuru sana Rais hakuweza kutuacha katika kadhia hii ya mafuriko.
“Hapa tuliposimama mto ulihama njia yake na kuingia katika eneo la msufini na kusababisha madhara makubwa, Tulichokifanya hapa ni hatua za awali ili kudhibiti mafuriko yasifike katika makazi ya wananchi, ambapo gharama za kuchumbua na kuweka Tuta umegharimu zaidi ya milioni 30”. Alisema Prof, Kabudi.
Sambamba na hayo Prof, Kabudi alitoa shukrani za dhani Kiwanda cha Sukari cha Mkulazi chini ya Mtendaji Mkuu wa Kiwanda hicho kwa Kutoa Mtambo uliotumika kuchimbua mto na kupandisha Tuta litakalosaidia mafuriko kutofika katika makazi ya wananchi.
Nao baadhi ya Wananchi waliohudhuria kujionea ujenzi wa Tuta hilo walidai kukamilika kwa tuta hilo kumeweza kuwasaidia kutopata madhara ya mafuriko kwa mvua kubwa iliyonyesha jana (Aprili 4, 2024) kwani kwa ukubwa wa mvua hiyo ungeweza kuleta mafuriko katika makazi ya wananchi.
Leave a comment