Naibu Wazirj Mkuu, Dk. Doto Biteko amesema migodi zaidi ya 350 ya wachimbaji wadogo imeunganishwa na umeme wa gridi ya Taifa na hivyo kupunguza gharama za uzalishaji na kurahisisha shughuli mbalimbali za migodi. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Pia amesema hadi sasa baadhi ya migodi mikubwa ikiwemo Geita Gold Mines Limited (GGML) na STAMIGOLD Biharamulo Mine ambayo ilikuwa haina umeme kwa muda mrefu sasa imeunganishwa na umeme wa gridi ya Taifa.
Dk. Biteko ametoa kauli hiyo leo Jumatano wakati akifungua kongamano la kimataifa la madini na uwekezaji Tanzania 2023 linalofanyika kwa siku mbili tarehe 25,26 Oktoba mwaka huu jijini Dar es Salaam.
Amesema Serikali inafahamu kuwa bado kuna mahitaji makubwa ya migodi kuunganishwa na umeme wa gridi ya Taifa hivyo inaendelea na kuboresha sekta hiyo.
“Napenda kuwahakikishia kuwa, kadri tunavyoimarisha uwezo wetu wa kuzalisha, kusafirisha na kusambaza umeme nchini, tutahakikisha migodi yote mikubwa na midogo inaunganishwa na umeme wa gridi ya Taifa.
“Pia Serikali inaendelea kuimarisha miundombinu ya usafirishaji ikiwa ni pamoja na ujenzi wa reli ya kisasa na barabara zinazounganisha maeneo yenye migodi na shughuli mbalimbali za madini ili kurahisisha usafirishaji wa bidhaa zinazoingia na kutoka migodini,” amesema.
Leave a comment