MGOGORO kati ya wafugaji na wakulima katika Kijiji cha Lembapuli, Wilaya ya Kiteto mkoani Manyara umechukua sura mpya baada ya wakulima kudaiwa kuvamia makazi ya wafugaji na kushambulia mifugo kwa risasi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Wakizungumza kwa nyakati tofauti kwa njia ya simu na MwanaHALISI Online baadhi ya wahanga wa tukio hilo wamedai lilifanyika saa 6.00 usiku wa kuamkia leo Ijumaa, ambapo watu wanaodaiwa kuwa wakulima walivamia makazi na kuanza kushambulia kwa risasi.
Mmoja wa wahanga wa tukio hilo, Sanyakwa Kapande, amedai watu hao walivamia nyumba yake kisha kuvunja milango na kuvamia zizi la ng’ombe, ambapo baadae walishambulia kwa risasi ng’ombe kadhaa.
“Wengine waliingia katika zizi la ng’ombe wakaenda kupiga risasi ng’ombe 10 kati yao mmoja amekufa wengine wamejeruhiwa vibaya sidhani kama watapona kwa sababu wamepigwa risasi tumboni na kuvunjwa miguu,” amedai Kapande.
Alipoulizwa chanzo cha tukio hilo, Kapande amedai ni mgogoro wa ardhi kati ya wafugaji na wakulima, ulioibuka tena baada ya kusuluhishwa na mamlaka ya Kijiji.
“Nahisi shida ni mgogoro wa ardhi, hapo nyuma tulisuluhushwa na kuambiwa wafugaji tulipe fidia baada ya ng’ombe zetu kuvamia mashamba, tulilipa ukaisha, lakini tunashangaa wamerudi tena,” amedai Kapande.
Naye Tilian Naisendu, amedai “hapa kuna mgogoro wa muda mrefu sana watu wanagombea mipaka Serikali ilikuja kutafuta chanzo tatizo wakaja kupima na kugawa maeneo ikawaondoa wakulima lakini wakulima hawataki kuondoka maeneo waliyotengewa wafugaji.”
MwanaHALISI Online imemtafuta Kamanda wa Jeshi la Polisi Manyara, George Katabazi, kwa ajili ya kupata ufafanuzi wa tukio hilo, ambaye amesema kwa sasa wanafanya uchunguzi kujua chanzo chake.
“Nipo kwenye kikao lakini taarifa hizo ni za kweli,” amesema.
Chanzo bado kinachunguzwa hata hivyo eneo hilo kuna mgogoro wa ardhi kati ya wakulima na wafugaji. Taarifa za awali ng’ombe tisa wamejeruhiwa na mmoja kufa au kuuawa,” ameandika Kamanda Katabazi katika ujumbe mfupi.
Leave a comment