JUMLA ya abiria 17 kati ya 27 waliozama na meli ya MV Maman Benita kwenye Ziwa Tanganyika, wameokolewa huku juhudi za kuendelea kuwatafuta wengine zikiendelea. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Taarifa iliyotolewa leo Jumatatu na Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) imesema meli hiyo ilianza safari yake tarehe 6 Aprili 2024 majira ya saa 12:00 jioni ikitokea bandari ya Kigoma kuelekea Kalemie, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Kati ya abiria 27, watanzania walikuwa watano, raia wa China wanne, raia wa Kongo 16 na raia mmoja wa Kenya pamoja na mtoto mdogo.
TASAC imesema meli hiyo iliyosajiliwa chini ya bendera ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, inamilikiwa na kampuni ya Kikongo, itwayo Etablissement Manimani.
“Meli hiyo iliyotarajwa kuwasili Kalemie majira ya saa 8:00 usiku, haikufika ambapo asubuhi ya tarehe 7 Aprli 2024, wavuvi walifanikiwa kumwokoa abiria mmoja mwenye
asili ya China na kisha kutoa taarifa kwa Mamlaka za Serikali ya Kongo juu ya kuzama kwa meli ya MV Maman Benita katika eneo la Kabimba, nchini Kongo.
“Baada ya kupata taarifa hiyo, zoezi la utafutaji na uokoaji lilianza mara moja ambapo hadi kufikia majira ya saa 1:00 usiku wa tarehe 7 April, 2024, wahanga 17 walikuwa
wameshaokolewa, kati yao ikijumuisha Wachina wawili, Watanzania watatu na Wakongo 12,” imesema.
Aidha, imesema chanzo cha kuzama kwa meli bado hakijajulikana isipokuwa Nahodha wa meli hiyo ameokolewa na timu ya wataalam tayari imekwenda eneo la tukio kwa ajli ya ufuatiiaji huku zoezi la utafutaji kuokoa abiria waliosalia linaendelea.
“TASAC inaendelea kutoa rai kwa wamiliki na waendeshaji wa vyombo majini kuzingatia Sheria na Kanuni za udhibiti usafiri majini na kuhakikisha chombo kina kuwa na majaketi okozi ya kutosha na kwa vyombo vidogo kuhakikisha abiria wanavaa jaketi okozi wakati wote wa safari ili kujiepusha na maafa yanayoweza kusababishwa na tukio la ajali.
“Aidha, TASAC inatoa pole kwa waathirika pamoja na familia kwa ujumla na taarifa kamili juu ya ajali hi itatolewa,” imesema taarifa hiyo.
Leave a comment