WAZIRI wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mohammedi Mchengerwa amesema kifo cha muigizaji mkongwe Chuma Suleiman maarufu kama Bi Hindu kimeacha pengo kubwa kwenye tasnia hiyo kwa kuwa alikuwa mwalimu na mlezi aliyeacha alama kwa wasanii wenzake. Anaripoti Faki Ubwa, Dar es Salaam … (endelea).
Mchengerwa ametoa kauli hiyo jana tarehe 10 Julai, 2022 wakati akitoa salamu za rambirambi kwa familia ya Bi Hindu kwa niaba ya serikali katika mazishi ya msanii huyo yaliyofanyika Magomeni jijini Dar es Salaam.
Amesema vilevile Rais Samia Suluhu Hassan ameshtushwa na msiba huo hasa ikizingatiwa Bi Hindu alikuwa mmoja wa wasanii waliokuwa kinara kuelimisha jamii kwa mambo mbalimbali.
“Bi Hindu alitoa elimu kupitia sana yake na Rais Samia amepatwa na mshtusho, zipo ahadi nyingi kwa wasanii lakini kifo ni ahadi isiyokwepeka.
“Bi Hindu anafariki katika kipindi ambacho Serikali ya Rais Samia inafanya Mapinduzi kwenye tasnia ya Sanaa tasnia ya filamu. Leo tunapozungumza tunasiku kama nane au Tisa nchi yetu ikitambuliwa kwenye tuzo kubwa duniani Tuzo za Hoollwood” amesema Mchengerwa.
Aidha, naye Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Shaka Hamad Shaka ametoa pole kwa niaba ya Chama hicho kwa wafiwa wote.
“Bi Chuma alikuwa mwalimu, mlezi mtoa matumani na ameacha alama kwa kizazi kijacho mchango wake mkubwa tutaukumbuka” amesema Shaka.
Bi Hindu amefariki dunia tarehe 9 Julai, 2022 baada ya kuugua kwa muda wa zaidi ya miaka miaka mitatu.
Bi Hindu anadaiwa kuwa na watoto 11 ambapo mpaka umauti unamfika, walikuwa wamebaki watoto wanne, kati ya wakike watatu na wakiume mmoja.
Leave a comment