BENKI ya NMB nchini Tanzania imezindua mpango maalum wa mikopo yenye riba nafuu kwa walimu kuwawezesha kumudu gharama ya elimu kwa watoto wao, kujiendeleza kitaaluma, kununua vyombo vya usafiri na kulipia bima. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Aidha kifurusho hicho maalumu kwa walimu kitamwezesha Mwalimu kukopa kwa riba nafuu na kuweza kufanya shughuli mbalimbali ikiwemo za kilimo, elimu na biashara.
Uzinduzi wa kifurushi hicho umefanyika mwishoni mwa wiki iliyopita kwa nyakati tofauti katika Mikoa ya Kilimanjaro, Mwanza, Manyara pamoja na Arusha.
Akiwa Mkoani Mwanza Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi na Biashara NMB, Filbert Mponzi alisema kupitia kifurushi cha “Mwalimu Spesho” walimu nchini wataondokana na adha ya mikopo ya mitaani yenye riba kubwa.
“Kupitia kifurushi cha Mwalimu Spesho, walimu watakopa kulipia gharama za elimu kwa watoto au kujiendeleza wenyewe kitaaluma kwa riba nafuu ya asilimia 10,” alisema Mponzi
Kupitia kifurushi hicho, walimu pia watakopa kwa ajili ya shughuli za kilimo kwa riba ya asilimia tisa pamoja na kukopa kwa ajili ya kununua vyombo vya usafiri ikiwemo pikipiki na kulipia bima.
Kabla ya kupokea mikopo, Mponzi alisema walimu hao watapewa bure elimu ya fedha kuwaepusha na matumizi yasiyo ya lazima ili kuhakikisha mikopo hiyo inatumiwa kwa maelengo yaliyokusudiwa.
Naye Mkuu wa kitengo cha wateja binafsi NMB, Aikansia Muro akizungumza na walimu wa Mikoa ya Arusha, Manyara na Kilimajaro alisema NMB imekuwa ikifanya siku ya Mwalimu kila mwaka na huu ukiwa ni mwaka wa kumi, ambayo huenda sambamba na kutoa elimu ya kifedha.
Muro alisema wamekuja na mpango huo maalumu kwa ajili ya walimu na umelenga kuangalia huduma zote za muhimu ambazo zinalenga kujibu changamoto zote mwalimu anazopitia na mahitaji yake muhimu.
Alisema wamefikia hatua ya kuja na mpango huo baada ya benki hiyo kufanya utafiti na kuweza kugundua changamoto wanazopitia walimu hao ambapo walimu hao wataweza kukopa fedha kupitia mkopo wa elimu wenye riba ya asilimia 10 na kuweza kufanya maswala mbalimbali ikiwemo kujiendeleza mwenyewe au kumwendeleza mtoto wake .
“Mpango huo umebeba bidhaa za mikopo yenye riba nafuu ikiwemo ya kujiendeleza kielimu ,mkopo wa kuendeleza biashara ndogondogo, mkopo wa kilimo ambao unaangalia mnyororo wa thamani wenye riba ya asilimia 9, mkopo wa vifaa vya ujenzi ,vyombo vya moto ikiwemo bodaboda na pikipiki ya miguu mitatu na malengo makuu yakiwa ni kumwezesha Mwalimu kunufaika na uwepo wa benki yetu kwa gharama nafuu,” alisema Muro.
Mkuu wa mkoa wa Mwanza, Robert Gabriel aliipongeza NMB kwa kutoa mikopo yenye riba nafuu kwa walimu akisema itawakomboa kutoka kwenye mikopo ya riba kubwa inayotolewa na watu binafsi mitaani.
Nawasihi walimu watumie vema fursa ya mikopo kuanzisha miradi ya ujasirimali kujiongezea kipato bila kuathiri utendaji wala kuingilia muda wa kazi,” alisema Gabriel huku akizihimiza taasisi za fedha kuhakikisha zinatoa huduma jumuishi kwa wananchi wa kada zote hadi vijijini.
Kwa upande wake, Mmoja wa walimu, Salome Gwandu alisema wanashukuru benki hiyo kwa kuja na kifurushi hicho cha kipekee kwa kuwakumbuka walimu kwani walikuwa wanakabiliwa na changamoto kubwa ya kutozwa riba ya asilimia 14 hadi 16 ambapo kwa sasa imekuwa ni pungufu kwao na wapo tayari kuchangamkia fursa hiyo.
Mbali na kutangaza neema hiyo kwa walimu, Neema kupitia makongamano hayo ilitoa elimu ya kifedha na Ujasiriamali kwa zaidi ya 1,500 ambao ni wawakilishi kutoka mikoa yote ili waweze kuziona fursa zinazowazunguka na kijiongezea kipato.
Leave a comment