OFISI ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma nchini Kenya imesema Mbunge wa Kimilili, Didmus Barasa ataendelea kusota rumande kwa siku 10 zaidi kusubiri upelelezi wa kesi inayomkabili ya mauaji. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Mbunge huyo kupitia chama cha UDA, tarehe 12 Agosti, 2022 alijisalimisha kwa vyombo vya usalama nchini humo, siku moja baada ya kitengo cha upelelezi wa jinai DCI kutangaza msako dhidi yake kwa tuhuma za mauaji ya mlinzi wa mshindani wake wa kisiasa, Brian Kahemba.
Barasa, anatuhumiwa kwa mauaji ya Brian baada ya kumpiga risasi paji la uso na kumuua papo hapo Jumanne, Agosti 8, eneo la Chebukwabi huko Kimilili, kaunti ya Bungoma nchini humo.
Hatua hiyo imekuja baada ya upande wa mashtaka kuomba muda zaidi wa kuwaruhusu wapelelezi kukamilisha uchunguzi na kuruhusu mashahidi zaidi wakiwemo maafisa wa Shirika la Vijana wa Huduma kwa Taifa (NYS) na Tume huru ya uchaguzi na mipaka nchini humo (IEBC) kukusanya taarifa za kutosha.
Mahakama iliamua kwamba wapelelezi pia walihitaji muda wa kukamilisha na kuwasilisha ripoti za uchunguzi na mwili na wa silaha iliyotumika katika mauaji.
Kesi hiyo itatajwa tena tarehe 24 Agosti 2022 kwa Mwendesha mashtaka wa Serikali – DPP kuthibitisha hali ya upelelezi kabla ya kutoa uamuzi wa kushtakiwa.
Juzi Barasa alifikishwa katika Mahakama ya Bungoma kwa madai ya mauaji.
“Upande wa mashtaka ukiongozwa na Mkuu wa Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma Kanda ya Magharibi, Peter Kiprop ulituma maombi kwamba mbunge huyo abaki rumande ili kuruhusu ODPP ishirikiane na Shirika la Ulinzi la Mashahidi (WPA) ili kulinda mashahidi walioonyesha hofu ya kutoa ushahidi,” ODPP alisema.
Mshukiwa anawekwa kizuizini kabla ya uchunguzi kukamilika ili kuzuia aina yoyote ya kuingiliwa kwa mashahidi kama vile vitisho, madhara ya kimwili au hata kifo.
Wiki iliyopita Barasa aliwekwa katika mahabusu ya polisi iliyopo kwenye mjini Kisumu baada ya kukamatwa siku ya Ijumaa.
Alikimbizwa Kisumu kwa kile polisi walichokitaja kuwa usalama wake.
Hata hivyo, amekana madai kwamba alimpiga risasi na kumuua Brian Olunga katika kituo cha kupigia kura.
Leave a comment