RAIS wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Wallace Karia ameweka wazi kwamba yeye sio wanachama wala shabiki wa klabu ya Simba kama watu wengi wanavyosema na kukili kuwa yeye ni mwanachama wa klabu ya Coastal Union ya Tanga. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea)
Karia aliyazungumza hayo kwenye mkutano uliowakutanisha wadau wa mpira wa Miguu nchini kwa njia ya mtandao ambao pia ulimuhusisha Waziri wa Sanaa, Utamaduni na Michezo Mohammed Mchengerwa ambapo mada kuu ilikuwa ni kutazama usajili uliofanya na timu za Ligi Kuu Tanzania Bara kuelekea msimu mpya.
Akijibu swali aliloulizwa na kiongozi wa mdaharo huo, kuhusu kiongozi huyo kuhisiwa kuwa shabiki wa klabu ya Simba, Rais Karia alijibu kwamba mchezo wa mpira wa Miguu unaongozwa na viongozi ambao wanatoka kwenye klabu lakini kikubwa ni kuzingatia maadili katika kazi zao
“Mpira wa Miguu unaongozwa na viongozi ambao wanatoka kwenye klabu zao, mtu yeyote anayekuwa kwenye mpira wa miguu lazima atakuwa na klabu yake na mapenzi yake ila inatakiwa kiwango cha maadili kuwa juu kuliko ushabiki wake”. Alisema Karia
Aidha kiongozi huyo aliongezea kuwa yeye sio mwanachama wa klabu hiyo kama watu wanavyosema, na hata ile picha inayosambaa ambayo ilimuonesha akiwa amevaa jezi ya Simba alisema kuwa ni ya muda mrefu na alipewa wakati alipoenda kumuwakilisha kiongozi wake kwenye tamasha la klabu hiyo ambao walikuwa wakitimiza miaka 80.
“Mimi wala sio Mwanachama wa Simba mimi ni Mwanachama wa Coastal Union, na ile picha ni ya zamani, nilitumwa niende kwenye Simba Day kumuwakilisha kiongozi wangu wa kipindi hiko, nilivyofika pale nikapewa ile jezi nivae, lakini nilienda na nguo tofauti” alisisitiza Rais huyo
Ikumbukwe kiongozi huyo kwa sasa yupo kwenye kipindi chake cha pili cha uongozi toka alipochukua madaraka kutoka kwa mtangulizi wake Jamali Malinzi.
Leave a comment