MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, amesema ataongoza maandamano ya amani ya kudai katiba mpya, ili kumuenzi aliyekuwa mgombea wao wa urais katika Uchaguzi Mkuu wa 2015, Hayati Edward Lowassa, aliyelilia mifumo huru na ya haki katika uchaguzi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Maandamano hayo ya amani yanatarajiwa kufanyika kesho tarehe 15 Februari 2024, ikiwa taifa linaomboleza kifo cha Lowassa aliyekuwa waziri mkuu wa zamani, ambaye amefariki dunia tarehe 10 Februari mwaka huu na mwili wake unatarajiwa kuzikwa nyumbani kwao Monduli, jijini Arusha, Jumamosi ijayo.
“Kwa mapenzi ya Mungu, nitaongoza maandamano ya taifa ya amani jijini Mwanza, taifa likiwa katika maombolezo ya hayati Lowassa. Lowassa aliamini sana katika kazi na alisisitiza salaam za hongera kwa kazi badala ya pole kwa kazi. Tunamuenzi kwa kuendeleza maombolezo pamoja na kazi,”
“Alijaribu kwa kuungana nasi mwaka 2015, akawa Mgombea wetu wa Urais na akawa mhanga wa wizi wa kura na mifumo isiyo ya haki katika uchaguzi. Taifa bado linalilia Katiba mpya na mifumo huru na ya haki ya Uchaguzi,” ameandika Mbowe katika ukurasa wake wa Twitter.
Mbali na kuongoza maandamano hayo kudai katiba mpya na tume huru ya uchaguzi, Mbowe amesema yanalenga kupaza sauti za wananchi kwa watawala juu ya changamoto za ugumu wa maisha.
“Taifa lina vilio vingi. Watawala wanapaswa kulitambua hili. Ni wajibu wetu kwa pamoja tupaze sauti zetu usiku na mchana hadi wenye mamlaka watambue hali halisi ya hisia za Umma wa Watanzania,” ameandika Mbowe na kuongeza:
“Maumivu yetu makubwa ni umasikini unaotesa maelfu kwa maelfu ya Watanzania kunakosababishwa na kupanda kwa viwango visivyohimilika vya gharama za maisha ikiwemo chakula, pembejeo, nauli, mgao mkubwa usioelezeka wa umeme nk Watanzania wote tukutane Mwanza tukaandike historia.”
Leave a comment