MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Taifa, Freeman Mbowe amekitaka Chama Cha Mapinduzi (CCM), kiikabidhi Chadema Serikali kama kimeshindwa kusimamia rasilimali za nchi kwa maslahi ya wananchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Shinyanga…(endelea).
Mbowe ametoa wito huo leo tarehe 28 Agosti 2023, katika mkutano wa hadhara wa Chadema, uliofanyika Kishapu mkoani Shinyanga, wakati akizungumzia mkataba wa uwekezaji wa bandari, uliofungwa kati ya Serikali ya Tanzania na Imarati ya Dubai.
Mwanasiasa huyo amehoji iwapo kama CCM imerogwa, hadi kupelekea kutaka kukabidhi uendeshaji wa bandari nchini kwa kampuni ya kigeni ya Dubai Port Wolrd (DP Wolrd), wakati rasilimali hiyo ni lango la uchumi wa nchi kwa kuwa inategemewa na nchi jirani zisizokuwa na bandari.
“Wanataka kumpa mwarabu bandari zote kwa mkataba wa milele, tunauliza Serikali yetu mnampaje mgeni? Nchi jirani zinaitegemea bandari ya Tanzania, lakini tunachukua bandari zetu mnamkabidhi milele, tunawauliza CCM mmerogwa?,” alisema Mbowe.
Mbowe amesema “Kama mmerogwa mmerogwa huyo aliyewaroga labda kafa. Mnakwendaje kugawa rasilimali na urithi wa nchi yetu? Mnasema bandarini kuna wizi tumeshindwa kuendesha. Tunawaambia CCM kama wameshindwa kuendesha bandari zetu waikabidhi serikali kwa Chadema tuna uwezo wa kuendesha bandari zetu kwa kutumia watanzania wetu.”
Katika hatua nyingine, Mbowe amedai Serikali ya CCM imeshindwa kutumia kikamilifu rasilimali za nchi, ikiwemo madini na gesi kwa ajili ya kuwaletea maendeleo wananchi wake, huku akidai wananchi waishio katika mikoa yenye rasilimali hizo wanaongoza kwa kuwa masikini.
Katika nyakati tofauti, Serikali imetoa ufafanuzi juu ya dosari zinazoibuliwa na wapinzi dhidi ya mpango wake wa kuipa DP World kazi ya kuendesha baadhi ya maeneo ya Bandari ya Dar es Salaam, ambapo imesema kampuni hiyo haitapewa mkataba wa milele, kama inavyodaiwa.
Leave a comment