FREEMAN Mbowe, Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Upinzani Tanzania- Chadema, amempongeza Rais wa nchi hiyo, Samia Suluhu Hassan, kwa kauli zenye upatanishi alizozitoa akiwa nchini Kenya. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Rais Samia, alikuwa na ziara rasmi ya kikazi ya siku mbili, tarehe 4 na 5 Mei 2021, Kenya kwa mwaliko wa Rais wa nchi hiyo, Uhuru Kenyatta.
Katika ziara hiyo, Rais Samia na mwenyeji wake, Rais Kenyatta, waliteta masuala mbalimbali ikiwemo kuimalisha ushirikiano baina ya mataifa hayo mawili ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Pia, marais hao, walifungua Jukwaa la Wafanyabiashara wa Tanzania na Kenya jijini Nairobi na baadaye Rais Samia akahutubia Mabunge Mawili ya Kenya- Bunge la Taifa pamoja na Bunge la Senate.
Miongoni mwa marais hao waliyokubaliana ni kuondoa vikwazo na kumaliza changamoto mbalimbali zinazokwamisha wafanyabishara kwenye mataifa hayo mawili pamoja na kuweka msimamo wa kutoruhusu watu kuwagombanisha.
Kutokana na hayo, Mbowe ametumia ukurasa wake wa Twitter, kuzungumzia ziara hiyo akisema “Kauli patanishi na unganishi za Rais Samia Suluhu Hassan, nchini Kenya zimeleta tabasamu pande zote mbili za nchi zetu.”
“Dunia imeona, imesikia na inasubiri vitendo. Hongera Mama. Tanzania uharibifu ni mkubwa zaidi. Rejesha tabasamu la Haki, Uhuru na Demokrasia. Tunakusubiri,” ameandika.
Kauli patanishi na unganishi za Rais @SuluhuSamia nchini Kenya zimeleta tabasamu pande zote mbili za nchi zetu. Dunia imeona, imesikia & inasubiri vitendo. Hongera Mama. Tanzania uharibifu ni mkubwa zaidi. Rejesha tabasamu la Haki, Uhuru na Demokrasia. Tunakusubiri. #NeverAgain
— Freeman Mbowe (@freemanmbowetz) May 5, 2021
Tayari Rais Samia, amekwisha weka bayana dhamira yake ya kukutana na viongozi wa vyama vya siasa nchini humo, ili kujadiliana njia bora za kuimalisha demokrasia na utawala bora.
Pia, Rais Samia amekubali barua ya Mbowe aliyoiwasilisha kwake, akiomba wakutane na Chadema wamenukuliwa wakisema, wanasubiri tarehe watakayopangiwa ya kwenda kuonana naye.
Leave a comment